Umoja wa Ulaya kusaidia Tanzania katika sekta ya kilimo na usafirishaji
Serikali ya Tanzania imetiliana saini mkataba wa msaada wa zaidi ya Shilingi Bilioni
134 sawa na Euro milioni 59.5 kutoka Umoja wa Ulaya (EU) kusaidia sekta ya kilimo
na usafirishaji nchini. Mkataba huo ulisainiwa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Dkt.
Servacius Likwelile kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na Balozi wa EU nchini Tanzania
Filberto Sebregond Alhamisi, tarehe 8 Mei 2014Jijini Dar es Salaam.
Akizungumza
baada ya kutia saini mkataba huo, Dkt. Likwelile alisema kuwa sehemu ya msaada huo
ambao ni Shilingi Bilioni 82.4 ambazo ni sawa na Euro milioni 36.5 utatumika kuendeleza
sekta ya kilimo na kukuza uchumi nchini kwa kupitia kituo maalum cha uendelezaji kilimo
ukanda wa Kusini Tanzania (SAGCOT) na kuboresha miundombinu ya barabara za ukanda
huo.
Vilevile Dkt. Likwelile alisema kuwa sehemu iliyobaki ya msaada huo ambao
ni Shilingi Bilioni 51.9 ambazo ni sawa na Euro milioni 23 itatumika kuimarisha biashara
na ushirikiano katika jumuiya kwa kuanzisha kituo cha pamoja cha ukaguzi mipakani
(OSIS). “Vituo hivyo vya ukaguzi mipakani vitakuwa na manufaa si kwa Tanzania tu,
bali hata katika nchi mbalimbali zinazopakana na Tanzania” alisema Dkt. Lkwelile.
Alifafanua kuwa msaada uliosainiwa unamanufaa kwa wananchi kwa kuboresha miundombinu
vijijini na kusambaza umeme vitu ambavyo vitasaidia kukuza uchumi na kupunguza umaskini
nchini.
Naye Balozi wa EU nchini Filberto Sebregond alisema kuwa anaamini
msaada huo utasaidia juhudi za Serikali ya Tanzania katika kuongeza nafasi za ajira,
kupungua kwa bei za bidhaa mbalimbali na kuendelea kukuza uchumi nchini. Balozi huyo
alisema kuwa EU inaamini kuwa ushirikiano wake na Tanzania utaendelea kuimarika kwa
kuhimiza maendeleo kwa pande zote mbili na amani ya watu wake. Hafla hiyo ya kusaini
mkataba ilihudhuriwa na wawakilishi kutoka Wizara ya Fedha, Nishati na Madini, Uchukuzi
na Ujenzi, EAC, DFID, SAGCOT, wajumbe kutoka EU, Shirika la maendeleo ya Ufundi kutoka
Ubelgiji na washirika wa maendeleo.