Mkakati wa kimataifa wa kupambana na ujangiri hifadhi za wanyamapori!
Mkuu wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Helen Clark, atafanya ziara
nchini Tanzania kuanzia Mei 10 hadi 13, 2014. Wakati wa ziara yake, Helen Clark atakuwa
mgeni rasmi katika chakula cha jioni cha kufunga mkutano kuhusu ujangili wa meno ya
tembo na hifadhi ya wanyamapori hapo Mei 10, 2014, katika Hoteli ya Hyatt Regency
Kilimanjaro.
Ujangili wa meno ya tembo na biashara haramu ya pembe za ndovu
ni masuala yanayotia wasiwasi mkubwa barani Afrika na kwingineko, pamoja na kukua
kwa masuala ya kiusalama, kiuchumi, kisiasa na kimazingira bado uhalifu huu unaongezeka
kwa kasi. Katika Afrika Mashariki, makundi ya uhalifu yanatumia mbinu za kisasa kuua
tembo na kutumia fursa ya rushwa kuvusha pembe nje ya mipaka ya Afrika. Tanzania ni
nchi yenye idadi kubwa zaidi ya Tembo katika Afrika na ndio hasa iliyoathirika kwa
namna ya pekee na ukuaji wa tatizo hili. UNDP imekuwa ikifanya kazi kwa karibu na
serikali ya Tanzania na wadau wengine katika hifadhi ya wanyamapori kushughulikia
changamoto hizi.
Akiwa nchini, mkuu huyu wa UNDP atashiriki katika kufunga
mkutano wa Dar es Salaam juu ya hatua za kukomesha ujangili wakati ambapo wadau wa
kitaifa watajadili na kukubaliana juu ya hatua za utekelezaji wa kukomesha ujangili
wa meno ya tembo na biashara haramu katika bidhaa za wanyamapori. Mkutano huo utakuwa
wa kwanza kitaifa kufuatia mikutano ya kimataifa iliyofanyika Botswana, Paris na London.
Helen Clark pia atatembelea Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kushuhudia matokeo ya
mapambano dhidi ya jitihada za kupambana na ujangili zinazofanywa na UNDP na Mfuko
wa Dunia wa Mazingira zinazolenga uhifadhi wa wanyamapori na kutunza mazingira hususan
katika maeneo ya Kusini ya Tanzania, ikiwa ni pamoja na maeneo ya hifadhi ya Ruaha,
Kitulo, Mpanga Kipengere na Mlima Rungwe. Mkuu huyo wa UNDP ambaye pia ni Waziri
Mkuu wa zamani wa New Zealand, Helen Clark atamtembelea Spika wa Bunge, Mhe. Anne
Makinda (Mbunge) na kufanya mazungumzo na Wabunge Wanawake mjini Dodoma Mei 12, 2014,
ambapo atazungumzia masuala ya jinsia na maendeleo ya wanawake katika uongozi na siasa.
Tarehe
13 Mei, atakuwa Jijini Dar es Salaam na atatoa hotuba ya ufunguzi kwenye mkutano wa
Kamati ya UNDP ya Mradi wa Uwezeshaji wa Kidemokrasia (wenye thamani ya dola za Kimarekani
milioni 26), hususan suala la kura ya maoni kuhusu katiba mpya na uchaguzi mkuu wa
mwaka 2015 kwa ujumla. Kamati hiyo inaongozwa na wenyeviti wawili wa tume za uchaguzi
Tanzania (NEC na ZEC) na inajumuisha vyama vya kiraia, serikali, na wawakilishi wa
wafadhili.
Akiwa Tanzania, Helen Clark pia atakutana na viongozi waandamizi
wa serikali na vyama vya kiraia kujadili masuala ya ukuaji wa uchumi. Vilevile kutakuwa
na mkutano na waandishi wa habari Jumamosi tarehe10 Mei, 2014 majira ya jioni.