2014-05-08 08:13:54

Ujumbe wa Papa Francisko kwa Siku ya 51 ya Kuombea Miito Mitakatifu!


Neno la Mungu linasema kwamba, Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuhubiri Habari Njema ya Wokovu, na kuponya magonjwa yote na udhaifu wa kila aina. Na alipowaona makutano aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasiokuwa na mchungaji. Ndipo alipowaambia wanafusi wake “mavuno ni mengi lakini watenda kazi ni wachache”. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Siku ya 51 ya Kimataifa kwa ajili ya Kuombea Miito Mitakatifu inayoadhimishwa, tarehe 11 Mei 2014, Jumapili ya Kristo mchungaji mwema, inayoongozwa na kauli mbiu “Miito, ushuhuda wa ukweli” anasema, sehemu hii ya Maandiko Matakatifu inashangaza kwani kabla ya kupata mavuno mengi kuna haja kwanza kabisa ya kutayarisha shamba, kupanda na kulitunza, lakini kazi hii kubwa ndani ya Kanisa inafanywa na Mwenyezi Mungu na kwamba, shamba linalozungumzwa na Kristo ni mwanadamu, yaani ni Wakristo.

Mwenyezi Mungu ndiye kiini cha mavuno mengi kutokana na neema na umoja unaojionesha kati ya Mwenyezi Mungu na waja wake. Yesu anawaalika wafuasi wake kuomba ili watendakazi waweze kuongezeka katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu. Hawa ndio “washiriki wa Mungu” wanaojitosa kimasomaso kwa ajili ya Injili ya Kanisa.

Kwa mtu aliyeguswa na neema ya Munguinayookoa kama ilivyokuwa kwa Mtume Paulo anatambua kwamba, chemchemi ya miito yote mitakatifu ndani ya Kanisa ni neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba, waamini wenyewe ndilo “shamba la Mungu”. Hii ni kazi inayoweza kufanywa na Mwenyezi Mungu peke yake kwa kuonesha moyo wa shukrani kwa njia ya upendo na hatimaye, kumwabudu Mungu kutokana na matendo yake makuu aliyomkirimia mwanadamu, jambo ambalo anasema Baba Mtakatifu linahitaji uhuru wa mtu binafsi.

Waamini mara nyingi sana wamesali na kuimba kwamba, wao ni mali ya Mungu, watu na kondoo wa malisho yake na kwamba, Mwenyezi Mungu amemchagua Yakobo na Israeli kuwa mali yake mwenyewe. Kwa hakika waamini ni mali yake Mungu si kwa vile anataka kuwafanya kuwa watumwa la hasha! Lakini wanaunganishwa na Agano la milele na kwamba, upendo wake wadumu milele. Nabii Yeremia anawakumbusha waamini kwamba, Mwenyezi Mungu anachunga wito wa kila mtu ili Neno la Mungu liweze kutimia ndani mwake kama ufito wa mlozi, kielelezo cha maisha mapya. Kila kitu kinatoka kwa Mwenyezi Mungu ni ni zawadi ya Mungu kwa waja wake: dunia, maisha, kifo, hali ya sasa na ile ijayo na Mtume Paulo anawakumbusha waamini kwamba wao ni Wakristo na Kristo ni wa Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema waamini ni mali ya Mungu kutokana na uhusiano wa pekee walionao na Kristo unaojikita katika Sakramenti ya Ubatizo, inayowakirimia kuwa na maisha mapya. Kristo anaendelea kuwaongoza wafuasi wake, wao wanapaswa kumwamini na kumpenda kwa moyo, akili na nguvu zote. Kila wito unamchangamotisha mwamini kufanya hija inayomwondoa kutoka katika ubinafsi wake, ili kujishikamanisha na Yesu pamoja na Injili yake.

Waamini wanapaswa kufikiri na kutenda kadiri ya mapenzi ya Mungu, iwe ni katika wito wa maisha ya ndoa na familia, maisha ya kuwekwa wakfu au wito wa kipadre. Hii ni safari inayomwezesha mwamini kumwabudu Kristo kwa njia ya huduma makini kwa Kristo pamoja na jirani. Kumbe, waamini wote wanaalikwa kumwabudu Kristo kutoka katika undani wa mioyo yao sanjari na kuacha nafasi kwa neema inayofumbatwa katika Neno la Mungu, ikue na kuwaletea mabadiliko katika huduma makini kwa jirani.

Baba Mtakatifu anasema, waamini hawana haja ya kuwa na wasi wasi kwani Mwenyezi Mungu anafuatilia kwa ukamilifu kazi ya mikono yake na katika kila hatua ya maisha na kamwe hawezi kuwatelekeza! Yesu moyoni mwake anataka kutekeleza mpango alionao juu ya maisha ya kila mwamini na anataka kutekeleza mpango huu kwa kuzingatia utashi na ushiriki wa kila mwamini.

Papa Francisko katika ujumbe wake kwa Siku ya 51 ya Kuombea Miito Mitakatifu anaendelea kusema kwamba, hata leo hii Kristo anaishi na kutembea katika uhalisia wa maisha ya waamini wake; anafanya hija na maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; anaponya magonjwa na kuendelea kutembea na wagonjwa. Baba Mtakatifu anawalika waamini kusikiliza kwa makini sauti ya Kristo ili kutambua ni wito gani ambao Mwenyezi Mungu anawataka kuuishi, kwani maneno yake ni roho na maisha; wawe tayari kutenda kila jambo ambalo Kristo anawaambia.

Waamini wanachangamotishwa kufanya hija ya kijumuiya, ili kupata nguvu inayohitajika. Wito ni tunda linaokomaa katika shamba lililotayarishwa vyema katika upendo unaomwilishwa kwenye huduma na katika uhalisia wa maisha ya Kanisa. Hakuna wito unaozaliwa katika ubinafsi na kwa ajili ya masuala binafsi. Wito unabubujika kutoka katika moyo wa Mwenyezi Mungu na kukua katika watu waaminifu na wanaoonja upendo wa kidugu na kwa njia ya ushuhuda wa maisha na upendo wa kidugu, watu wengine wanaweza kuwatambua kwamba, wao kwa hakika ni wafuasi wa Kristo.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, hii ni changamoto inayowataka waamini wakati mwingine kufanya maamuzi magumu kwani wanaweza kukutana na vizingiti ndani na nje ya maisha yao, wanavyopaswa kuvishinda, kwani wakati mwingine Neno la Mungu linaweza kupokwa na Shetani; mahangaiko ya ndani, hali ya kukata tamaa pamoja na vishawishi vya malimwengu. Mambo haya yanaweza kuwakatisha wengi tamaa kwa kutafuta njia ya mkato, lakini waamini wanakumbushwa kwamba, furaha ya kweli inabubujika kutoka katika imani kwa Yesu Kristo ambaye ni mwaminifu na kwamba, waamini wanaweza kufanya hija pamoja naye na kuwa kweli ni wafausi na mashahidi wa upendo wa Mungu kwa kufungua mioyo kwa mambo makuu kutoka kwa Mwenyezi Mungu, hii ndiyo changamoto kwa Wakristo.

Baba Mtakatifu anawataka Maaskofu, Mapadre, Watawa, Jumuiya na Familia za Kikristo kuhakikisha kwamba, wanashiriki kuelekeza miito mitakatifu katika utakatifu wa maisha, kwa njia ya mifano bora na maisha adili yak ila mwamini. Vyama vya Kitume na watu binafsi wajitahidi kutoa msaada wa mali na mali kwa watu wanaojisikia kuwa na miito mitakatifu.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha Ujumbe wake wa Siku ya 51 ya Kimataifa ya Kuombea Miito kwa kuwataka waamini wote kujitahidi kuwa ni udongo mzuri kwa ajili ya kusikiliza, kupokea na kulimwilisha Neno la Mungu, ili liweze kuzaa matunda ajaa! Waendelee kujishikamanaisha na Kristo kwa njia ya Sala, Tafakari ya Neno la Mungu, Ekaristi Takatifu pamoja na Sakramenti nyingine zinazoadhimishwa na Mama Kanisa, kwa njia ya mshikamano wa kidugu.

Kwa njia hii, furaha ya kuwa ni wadau wa Mungu katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu unaojikita katika huruma na ukweli; haki na amani itaongezeka maradufu. Mavuno yatakuwa mengi kadiri ya neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwa njia ya unyenyekevu, kila mwamini ataweza kuipokea zawadi hii moyoni mwake.

Ujumbe huu umehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.