China na Tanzania kushirikiana zaidi katika masuala ya kiuchumi!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete jioni ya
Jumatano, Mei 7, 2014 amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Watu wa China, Mheshimiwa Li Keqiang. Katika mkutano uliofanyika kwenye Hoteli ya
Transcorp Hilton ya mjini Abuja nchini Nigeria ambako wote wawili wamefikia wakati
wanashiriki katika Kongamano la Uchumi Duniani Afrika (World Economic Forum - Africa),
viongozi hao wawili wamezungumzia, kimsingi, mambo yanayohusu uhusiano wa Tanzania
na China.
Katika mkutano huo, Rais Kikwete amemwomba Mheshimiwa Li Keqiang
kuisaidia Tanzania kuboresha mfumo wake wa kutunza na kuhifadhi nafaka kutokana na
ongezeko kubwa za uzalishaji wa nafaka, ambao unatokana na kukua kwa kilimo cha Tanzania.
Waziri Mkuu Li Keqiang amekubali ombi hilo la Tanzania kwa kumweleza Rais
Kikwete Waziri wa Serikali ya China ambaye atasimamia kutekelezwa kwa mradi huo mkubwa
kutokana na ongezeko kubwa la nafaka katika kilimo cha Tanzania. Rais Kikwete pia
amemwomba Waziri Mkuu huyo wa China kusaidia kuhakikisha kuwa kazi ya ujenzi wa Bandari
ya Bagamoyo inaanza mapema iwezekanavyo, ombi ambalo Waziri Mkuu Li Keqiang amelikubali.
Rais
Kikwete pia ameipongeza China kwa dhana yake iliyotangazwa karibuni ya 4-6-1 ambako
kuna misingi minne, maeneo sita ya kipaumbele na eneo moja la mwelekeo kama msingi
mkuu wa Siasa za Nje za Jamhuri ya Watu wa China. Rais Kikwete pia ameisifu China
kwa kusaidia maendeleo ya Afrika kwa kutoa misaada ya maendeleo, kuwekeza na kufanya
biashara na Bara la Afrika na pia kuiwezesha Afrika kupata teknolojia ya kisasa kutoka
China.
Aidha, Rais Kikwete ameishukuru China kuwekeza katika uchumi wa Tanzania,
akisema kuwa China ni moja ya wawekezaji wakuu katika uchumi wa Tanzania kwa kiasi
cha dola za Marekani bilioni 2.5. “Tunashukuru sana kwa uwekezaji wa kila aina, wa
mwisho mkubwa ikiwa ni kutupatia mkopo wa kiasi cha dola milioni 1.2 bilioni kwa ajili
ya ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar Es Salaam,” amesema Rais Kikwete
na kuongeza kumshukuru Waziri Mkuu kwa misaada ya kijeshi ambayo Tanzania inaipata
kwa China.“Nchi yetu inalindika vizuri zaidi kwa sababu ya misaada yenu.”
Naye
Waziri Mkuu Li Keqiang ameipongeza Tanzania kwa kuadhimisha miaka 50 ya Muungano wa
Tanganyika na Zanzibar na pia ameonyesha furaha yake kuona maendeleo ya kiuchumi ambayo
Tanzania inaendelea kuyapata. Amesema kuwa urafiki wa China na Tanzania siku zote
umekuwa msingi mkuu wa mahusiano ya China na Afrika na hali hiyo itaendelea kuwa ukweli
wa mahusiano baina ya China, Afrika na Tanzania.