Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi, mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye ofisi za
Umoja wa Mataifa mjini Geneva pamoja na ujumbe wake wanasema kwamba, Vatican inatoa
umuhimu wa pekee katika Mkataba dhidi ya ukatili, CAT kama chombo muhimu sana katika
mapambano dhidi ya vitendo vinavyodhalilisha utu na heshima ya binadamu.
Askofu
mkuu Tomasi ameyasema hayo siku ya Jumatatu tarehe 5 Mei 2014 alipokuwa anawasilisha
taarifa ya Vatican dhidi ya ukatili katika Tume ya Umoja wa Mataifa inayoendelea na
kikao chake mjini Geneva. Vatican iliridhia mkataba huu kunako tarehe 22 Juni 2002
ili kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu
mintarafu Azimio la Umoja wa Mataifa kuhusu haki msingi za binadamu.
Askofu
mkuu Tomasi anafafanua kwamba, Vatican kama nchi mwanachama inajikita kwa namna ya
pekee katika eneo la mji wa Vatican ambalo inaweza kutekeleza mamlaka yake kisheria,
kutokana na ufafanuzi huu, utekelezaji wa mkataba huu hauna budi kuangaliwa mintarafu
mji wa Vatican na viunga vyake. Ujumbe wa Vatican katika mkutano huu umefafanua hatua
za kisheria ambazo zimetekelezwa na Mji wa Vatican, kama sehemu ya utekelezaji wa
mapendekezo yaliyokuwa yametolewa kwenye mkataba wa kudhibiti ukatili.
Askofu
mkuu Tomasi amebainisha kwamba, Vatican haina mamlaka kisheria kudhibiti ukatili unaoweza
kufanywa na watoto wa Kanisa sehemu mbali mbali za dunia. Kila mwamini anayeishi katika
nchi fulani anawajibika na kuwajibishwa na sheria za nchi husika. Kutokana na mantiki
hii, kila serikali ina wajibu wa kulinda watu walioko chini ya mamlaka yake, kama
ilivyo Vatican kuwajibika kwa watu wanaoishi mjini Vatican mintarafu sheria zake.
Askofu mkuu Tomasi anasema, serikali za nchi husika zinawajibika kisheria
kuwashughulikia watu wote wanaovunja sheria na kusababisha nyanyaso na dhuluma katika
eneo lake. Kila mtu hata kama ni mwanachama wa taasisi zinazosimamiwa na Kanisa Katoliki
anawajibika kwa mamlaka halali ya nchi anamoishi.
Ni matumaini ya Askofu mkuu
Silvano Tomasi kwamba, utekelezaji wa mkataba dhidi ya ukatili unazingatia maeneo
yaliyobainishwa kwenye mkataba huo na wala si vinginevyo. Hii inatokana na ukweli
kwamba, ikiwa kama wanachama wataingiza mambo mengine nje ya mambo msingi yaliyobainishwa
kwenye mkataba, watakuwa wanakwenda kinyume cha asili na malengo yake na hivyo kuhatarisha
hali ya watu ambao wameteswa na kudhulumiwa. Kwa mantiki hii kazi ya tume itakuwa
inaonesha udhaifu mkubwa na hata pengine kukosa uhalali wa kuendelea kuwepo!