2014-05-06 06:57:47

Sakramenti ya kipaimara hukuza na kuzamisha neema ya Ubatizo!


Kwa njia ya Sakramenti ya Kipaimara muungano wa Wabatizwa na Kanisa hufanywa kuwa mkamilifu zaidi, kwani wanatarajirishwa kwa nguvu ya pekee ya Roho Mtakatifu na hivi hulazimika kwa nguvu zaidi kuieneza na kuitetea imani kwa maneno na matendo, kama mashahidi wa kweli wa Kristo na Kanisa lake. RealAudioMP3

Sakramenti ya Kipaimara hukuza na kuzamisha neema ya Ubatizo kiasi cha kuwafanya Wakristo wathubutu kumwita Mwenyezi Mungu, “Abba, yaani Baba”. Inawaunganisha zaidi na Kristo na kuwapatia mapaji ya Roho Mtakatifu ambayo Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuyatafakari katika katekesi zake za kila Jumatano zinazotolewa mjini Vatican.

Ni Sakramenti inayokamilisha kiungo cha kanisa na kuwapatia waamini nguvu na neema ya pekee ya kutetea imani kwa maneno, lakini zaidi kwa njia ya matendo yanayodhihirisha ushuhuda wa imani tendaji. Kwa njia ya Sakramenti ya Kipaimara, waamini wanaweza kukiri kwa ushujaa na ujasiri mkuu jina la Yesu na kamwe hawawezi kuuonea aibu Msalaba wa Kristo, kielelezo cha huruma, msamaha na upendo wa Mwenyezi Mungu kwa watu wake.

Wakristo wanaopokea Mapaji ya Roho Mtakatifu kwa njia ya Sakramenti ya Kipaimara, wanakumbushwa kwamba, wanapokea mhuri wa kiroho unaowawezesha kuwa na: roho wa hekima na akili; roho wa ushauri na nguvu; roho wa elimu na ibada pamoja na roho wa uchaji mtakatifu. Hivi ndivyo Askofu Beatus Kinyaiya wa Jimbo Katoliki Mbulu anavyowafundisha waamini wake 116 kutoka Parokia ya Roho Mtakatifu, Jimbo Katoliki la Mbulu wakati alipokuwa anatoa Sakramenti ya Kipaimara hivi karibuni Parokiani hapo.

Askofu Beatus Kinyaiya alitumia fursa hii kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Kanisa la Parokia ya Roho Mtakatifu, utakaogharimu kiasi cha shilingi za kitanzania millioni 915 hadi utakapokamilika.

Askofu Kinyaiya anaendelea kuwataka waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema nchini Tanzania kusali kwa ajili ya kuombea ufanisi na tija katika vikao vya Bunge Maalum la Katiba ili wajumbe waweze kutekeleza dhamana nyeti waliyotumwa kuifanya na watanzania wenzao walipowachagua kuwawakilisha Bungeni. Askofu Kinyaiya anasema, watanzania wengi hawafurahii kuona wala kusikia malumbano yasiyokuwa na tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya watanzania wote.

Kuna haja kwa Wabunge kubadilika na kuanza kuonesha dira na mwelekeo mpya katika mijadala ya kutunga Katiba mpya ya Tanzania. Watanzania wanahitaji mambo makuu matatu kwa sasa: Katiba Mpya itakayolinda: amani, umoja na mshikamano wa kitaifa, kwa ajili ya ustawi na maendeeleo ya watanzania wote. Watanzania wanahitaji Katiba ambayo kimsingi ni sheria mama itakayowaongoza katika mchakato wa maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii. Katiba itakayolinda na kudumisha haki msingi, utu na heshima ya binadamu pamoja na uhuru wa kuabudu.

Imeandaliwa na
Rodrick Minja,
Dodoma.







All the contents on this site are copyrighted ©.