Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake Jumanne, tarehe 6 Mei 2014 kwenye Kikanisa
cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican amewataka waamini kutolea ushuhuda wa
imani tendaji na uaminifu kwa Kristo na Kanisa lake, kwa kutambua kwamba, Kanisa ni
Mama.
Baba Mtakatifu amesimulia safari ya ushuhuda iliyooneshwa na Mtakatifu
Stefano, shahidi wa kwanza kuyamimina maisha yake kwa ajili ya imani kwa Kristo na
Kanisa. Ni ujasiri na ushujaa uliopelekea wivu kutoka wakuu wa Makuhani na waandishi
hata wakamtwanga kwa mawe hadi kufa! Ni kundi la watu lililokuwa linapingana na Roho
Mtakatifu kwani ndani mwao walikosa amani na utulivu na matokeo yake, mioyo yao ilisheheni
wivu na roho mbaya, matunda ya kazi ya Shetani katika maisha ya mwanadamu!
Kifodini
cha Stefano kinaonesha mapambano kati ya Mungu na Shetani na kwamba, Wakuu wa makuhani
walipania kuwadhulumu wafuasi wa Yesu ambao tayari walikuwa wamekwisha ambiwa na Yesu
mwenyewe kwamba, wangekumbana na madhulumu kwa ajili ya jina lake, lakini walikuwa
hawana sababu ya kusikitika, kwani kwa mwamini kuyamimina maisha yake ni sehemu ya
mchakato wa kumwilisha Heri za Mlimani, muhtasari wa Mafundisho Makuu ya Yesu. Madhulumu
yakipokelewa kwa imani ni chemchemi ya utakatifu ndani ya Kanisa na kielelezo cha
hali ya juu kabisa cha ushuhuda kwa Kristo na Kanisa lake.
Baba Mtakatifu anawakumbusha
waamini kwamba, wao ni wafuasi wa Kristo, wanaotakiwa kutolea ushuhuda wa imani tendaji
katika maisha yao hata kama itawabidi kujisadaka kwa kuyamimina maisha yao! Baada
ya mauaji ya Stefano shahidi, Kanisa lilikumbana na mkono wa chuma, kiasi cha kuwasambaratisha
Wakristo sehemu mbali mbali za dunia. Walidhani kwa kufanya hivi walikuwa wanazima
moto wa Injili, lakini kumbe sivyo!
Wakristo kila walipofika waliendelea kutangaza
Habari Njema ya Wokovu kwa kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake,
kwa hakika, damu ya Mashahidi imekuwa ni mbegu ya Ukristo sehemu mbali mbali za dunia.
Kuna haja kwa Wakristo kujisadaka kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa, kwa
kutambua kwamba, Roho Mtakatifu anaendelesa kufanya kazi ndani ya Kanisa.
Kwa
njia hii, Kanisa lina uhakika wa kutembea katika njia ya ukweli na haki, kwa kuzingatia
mambo msingi katika maisha, yaani ushuhuda wenye mvuto na mashiko. Wakristo wanapofanya
tafakari kuhusu ushuhuda wa imani ulioneshwa na Stefano pamoja na Wakristo waliokuwa
wanakimbia mateso na madhulumu wanapaswa kuchunguza dhamiri zao ili kutambua hali
yao ya maisha ya kiroho, kama kweli inazaa matunda yanayokusudiwa, yaani wongofu wa
ndani na ushuhuda wa maisha kama njia sahihi ya kumwilisha wito na maisha ya Kikristo!