2014-05-05 08:46:53

Uchaguzi mkuu Malawi, kumekucha!


Tume ya haki na amani, Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi, imetoa mafunzo maalum kwa kikundi cha watu 150 kitakachoshiriki katika kusimamia mchakato wa uchaguzi mkuu nchini Malawi, unaotarajiwa kufanyika hapo tarehe 20 Mei 2014. Wajumbe hawa wanaotoka katika Majimbo ya: Karonga, Mzuzu na Dedza, watapelekwa kwenye vituo vya kupigia kura na wakati wa kuhesabu kura ili kujidhirisha kwamba, uchaguzi mkuu nchini Malawi umefanyika kwa kuzingatia ukweli, uwazi na uhuru.

Tume ya haki na amani inawahamasisha waamini na wananchi wote wa Malawi katika ujumla wao kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika mchakato mzima wa uchaguzi, kama sehemu ya utekelezaji wa dhamana yao katika maendeleo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii. Wajumbe wametakiwa kuhakikisha kwamba, wanatumia ujuzi na maarifa waliyopata kutoka katika mafunzo haya, ili kutekeleza wajibu wao kama wasimamizi wa ndani, katika uchaguzi utakaovishirikisha vyama vikuu vitatu vya kisiasa nchini Malawi.

Wasimamizi wa ndani waliandaliwa na Tume ya haki na amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi wamejengewa uwezo wa kutambua kinzani za uchaguzi pamoja na kinzani zinazoweza kujitokeza katika utawala na mikakati iliyowekwa. Wadau mbali mbali watakaopewa dhamana ya kusimamia mchakato mzima wa uchaguzi wanapaswa kutekeleza kazi hii kwa weledi na dhamiri nyofu ili matokeo ya uchaguzi yaweze kupokelewa na wote, tayari kuanza mchakamchaka wa kuwaletea wananchi wa Malawi maendeleo endelevu.

Wasimamizi wa ndani ni waamuzi wanaotekeleza wajibu wao kwa niaba ya Tume huru ya uchaguzi nchini Malawi. Usimamizi makini, unaojikita katika ukweli na uwazi ni msaada mkubwa katika kuwaaminisha wapiga kura na viongozi wao kwamba, uchaguzi ulikuwa ni wa kweli, haki na uwazi.

Wasimamizi hawa pamoja na mambo mengine wamewezeshwa katika misingi ya haki na amani, uchaguzi na usimamizi bila ya kupendelea; changamoto za uchaguzi nchini Malawi kama zilivyobainishwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi.








All the contents on this site are copyrighted ©.