Mabalozi wa Vatican ni muhimu sana katika kukuza na kudumisha umoja na udugu
Baba Mtakatifu Francisko, tarehe 2 Mei 2014 majira ya jioni aliitembelea jumuiya Taasisi
ya Kipapa ya Wanadiplomasia wa Kanisa inayoundwa na Mapadre 29 kutoka katika nchi
16, wanaojiandaa kwa ajili ya kutoa huduma ya kidiplomasia kama wawakilishi wa Khalifa
wa Mtakatifu Petro sehemu mbali mbali duniani.
Baba Mtakatifu alipokelewa
na wakuu wa Jumuiya hii pamoja na kusali nao masifu ya jioni, baadaye Baba Mtakatifu
alizungumza na wanajumuiya hawa kama Baba na familia yake, akigusia masuala mbali
mbali ya maisha na utume wa Kanisa, lakini kwa namna ya pekee umuhimu wa majiundo
makini kwa viongozi wa Kanisa kwa sasa na kwa siku za usoni.
Baba Mtakatifu
anasema, kwa Mapadre wanaoandaliwa kuwa wanadiplomasia wa Kanisa sehemu mbali mbali
za dunia hawana budi kukazia mambo makuu matatu: weledi utakaowawezesha kutekeleza
dhamana na majukumu yao kwa ufanisi mkubwa, tija pamoja na kujiamini. Pili hawana
budi kujenga na kudumisha udugu unaoimarisha upendo na mshikamano katika maisha ya
Kipadre.
Tatu, wajenge utamaduni wa kusali na kufanya tafakari ya kina ya
Neno la Mungu pamoja na kudumisha Ibada ya kuabudu Ekaristi Takatifu itakayowasaidia
kuzungumza na Kristo kwa kumshirikisha matatizo, furaha na changamoto katika maisha
na utume wao.
Baba Mtakatifu amewataka Mapadre hawa wanaojiandaa kuwa wawakilishi
wa Vatican sehemu mbali mbali za dunia kujikita katika dhana ya unabii, kwa kuwa waaminifu
kwa Mwenyezi Mungu kwa kutambua historia ya ukombozi katika Agano la Kale na Agano
Jipya, kwa njia hii wataweza kuwatumikia vyema watu wa Mungu kwa nyakati hizi.
Baba
Mtakatifu anawataka kuwa makini kwa kusoma alama za nyakati, hali inayowataka kuwa
na weledi unaojikita katika ufahamu wa kina wa nchi wanayoitumikia. Ili kuweza kupata
ufahamu mkubwa kuna haja ya kujifunza, kutembelea na kuzungumza na wananchi husika.
Jambo la tatu kwa wanadiplomasia wa Kanisa ni kutekeleza wajibu wao kwa unyenyekevu.
Baba
Mtakatifu Francisko amekazia umuhimu wa wanadiplomasia wa Vatican sehemu mbali mbali
za dunia, ili kujenga na kudumisha umoja, udugu na mshikamano kati ya Khalifa wa Mtakatifu
Petro na Maaskofu mahalia pamoja na kutambua hatari wanazoweza kukumbana nazo wakati
wanatekeleza dhamana hii nyeti katika maisha na utume wa Kanisa. Kanisa litaendelea
kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu hata katika medani za
kimataifa.
Baba Mtakatifu amegusia pia maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu
kwa ajili ya familia itakayofanyika mjini Vatican mwezi Oktoba, 2014. Katika maongezi
yake, Papa amewasikiliza kwa umakini mkubwa Mapadre wanaojiandaa kutoa huduma za
kidiplomasia sehemu mbali mbali za dunia.