2014-05-05 08:36:33

Kanisa linaendelea kujizatiti kuwalinda na kuwatetea watoto


Mkutano wa kwanza wa Tume ya Kipapa ya kulinda watoto wadogo iliyokuwa na mkutano wake wa kwanza kuanzia tarehe 1- 3 Mei, 2014 ulikuwa na dhamana ya kutoa mapendekezo kwa Baba Mtakatifu Francisko kuhusu majukumu ya Tume hii pamoja na kuongeza wajumbe kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ili kuimarisha mikakati ya Kanisa katika kulinda na kuwatetea watoto wadogo.

Wajumbe hawa katika tamko lao la pamoja wanapenda kuonesha mshikamano wao wa dhati na wahanga wa nyanyaso za jinsia na kwamba, tangu mwanzo wa utume wao, wanapenda kutoa kipaumbele cha kwanza katika kulinda na kutetea watoto wadogo au watu wazima wakati wa kufanya maamuzi. Wajumbe wamepata fursa ya kueleza na kushirikisha mawazo, uzoefu na mang’amuzi pamoja na matarajio yao kwa Tume hii ya Kipapa.

Taarifa inasema, wajumbe wamejadiliana kulingana na maombi yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, kuhusu umuhimu na malengo ya Tume hii pamoja na kuwashirikisha watu wengine ili kuweza kuchangia utaalam wao. Wajumbe wamejadili jinsi ambavyo wanaweza kushirikiana na wataalam mbali mbali katika kulinda na kuwatetea watoto dhidi ya nyanyaso za kijinsia pamoja na kushirikiana na viongozi mbali mbali kutoka Sekretarieti ya Vatican. Matunda ya kazi hii yatawasilishwa kwa Baba Mtakatifu kwa ajili ya maamuzi zaidi.

Tume inapenda kuwahamasisha viongozi wa Makanisa mahalia kuibua mbinu mkakati utakaosaidia kuwalinda watoto wadogo kwa kwa kukazia: majiundo makini, elimu na jinsi ya kudhibiti nyanyaso za kijinsia. Kanisa linapenda kuwajibika kikamilifu katika kuzuia nyanyaso za kijinsia pamoja na kuwahudumia wahanga wa vitendo hivi pamoja na familia zao.

Kanisa kwa kushirikiana na watu wote wenye mapenzi mema, linapenda kuhakikisha usalama wa watoto dhidi ya nyanyaso. Wajumbe wanaomba sala katika utekelezaji wa majukumu yao kwa sasa na kwa siku za usoni.








All the contents on this site are copyrighted ©.