2014-05-02 14:05:28

Michezo ipewe hadhi na heshima yake kama chemchemi ya furaha, majiundo na ukomavu wa mtu!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 2 mei 2014 amekutana na kuzungumza na Timu ya Mpira ya Fiorentina na Napoli walioingia fainali ya Kombe la Italia pamoja na viongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Italia. Amewashukuru kwa kutambua dhamana na wajibu wao wa kijamii, kwani mpira wa miguu unawawajibisha wachezaji ndani na nje ya uwanja kama ilivyo kwa viongozi wa timu za mpira wa miguu katika ngazi mbali mbali.

Baba Mtakatifu amewakumbusha kwamba, alipokuwa kijana alipendelea sana kwenda kuangalia mpira wa miguu huku akiwa ameambatana na ndugu zake siku za jumapili, kwani haya yalikuwa ni matukio ya furaha, changamoto na mwaliko wa kufanya michezo iwe ni chemchemi ya furaha. Mchezo wa mpira wa miguu ni kitega uchumi kikubwa kwa wafanyabiashara wanaopeleka matangazo yao ya biashara na kwa vituo vya televisheni kama chanzo cha mapato.

Baba Mtakatifu Francisko anaonya kwamba, mwelekeo wa uchumi usipewe kipaumbele cha kwanza katika michezo kwani kitachafua mambo mengine katika ngazi mbali mbali. Michezo haina budi kupewa hadhi na heshima yake kwa kuhakikisha kwamba, wachezaji wanawajibika barabara, kwani wanatazamwa watu wengi, lakini sehemu kubwa ya mashabiki wao ni vijana, mwaliko wa kuwa na nidhamu na adabu njema kama wana michezo bora.

Baba Mtakatifu katika hotuba yake kwa wanamichezo na viongozi hawa anawakumbusha kwamba, michezo ina dhamana ya pekee katika elimu, malezi na ukomavu wa mtu kiroho, kimwili na kijamii; kwa kujenga na kuimarisha mshikamano, katika ukweli na heshima. Haya ndiyo mambo msingi ambayo mpira wa miguu unapaswa kuyaendeleza.







All the contents on this site are copyrighted ©.