2014-05-01 07:29:39

Mikutano ya Mabaraza ya Kipapa mjini Vatican


Mkutano wa Makardinai washauri wakuu wa Baba Mtakatifu Francisko katika mchakato wa mageuzi makubwa ndani ya Kanisa Katoliki umehitimishwa mjini Vatican siku ya Jumatano, tarehe 30 Aprili 2014. Mkutano huu umemaliza kimsingi kufanya tathmini na upembuzi wa kina kuhusu Mabaraza na Halmashauri za Kipapa.

Kardinali Lorenzo Baldisseri, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu, amewasilisha taarifa kuhusu mchakato wa maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayoadhimishwa Mjini Vatican, Mwezi Oktoba, 2014. Makardinali washauri wataendelea tena na kazi yao, mwanzoni mwa Mwezi Julai, 2014.

Ijumaa tarehe 2 Mei, 2014 kwa mara ya kwanza Baraza la Kipapa la Uchumi lililoanzishwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francisko, litafanya kikao chake mjini Vatican. Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kutoa hotuba elekezi wakati wa ufunguzi wa Baraza hili jipya. Ajenda kuu ya mkutano huu ni kuandika Katiba ya Baraza na ratiba elekezi ya kazi zitakazofanywa na Baraza hili, ili kuleta ufanisi na tija katika masuala ya uchumi mjini Vatican. Mkutano huu utafanyika kwa siku nzima ya Ijumaa.

Wakati huo huo, kuanzia Mei Mosi hadi tarehe 3 Mei, 2014 Tume ya Kipapa kwa ajili ya kulinda watoto inaanza mkutano wake wa kwanza tangu ilipoundwa na Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni. Wajumbe wanazungumzia kuhusu asili na malengo ya Tume hii pamoja na kuangalia uwezekano wa kuwashirikisha wajumbe wengine kutoka sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.