Watakatifu wapya, miamba ya huruma ya Mungu kukumbukwa kila mwaka ifikapo Mwezi Oktoba
Baada ya Baba Mtakatifu Francisko kuwatangaza Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo
II kuwa watakatifu, Jumapili tarehe 27 Aprili 2014 katika Ibada iliyohudhuriwa na
maelfu ya watu waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro
mjini Vatican pamoja na viunga vyake, watakatifu hawa wapya watakumbukwa kila mwaka
mwezi Oktoba kadiri ya Kalenda ya Liturujia ya Kanisa.
Kadiri ya Kalenda ya
Liturujia ya Kanisa kwa ajili ya kumbu kumbu ya Watakatifu, Yohane XXIII atakumbukwa
kila mwaka ifikapo tarehe 11 Oktoba. Hii ni siku maalum ambayo, kwa takribani miaka
hamsini iliyopita, Yohane XXIII alikuwa anafungua rasmi maadhimisho ya Mtaguso mkuu
wa Pili wa Vatican, tukio ambalo limeleta mabadiliko makubwa katika maisha na utume
wa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Hili ni tukio la kishujaa
lililomstahilisha Papa Yohane XXIII kuitwa Mtakatifu.
Mtakatifu Yohane Paulo
II atakumbukwa kila mwaka ifikapo tarehe 22 Oktoba. Hii ni siku ambayo Papa Yohane
Paulo II alipoanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, akaendeleza maadhimisho
ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican pamoja na kukazia umuhimu wa Mama Kanisa kujikita
katika mchakato wa Umissionari na Uinjilishaji Mpya. Mwezi Oktoba ni mwezi wa shughuli
na mikakati ya kimissionari ndani ya Kanisa.
Tangu sasa waamini na watu wenye
mapenzi mema wanaweza kuwaenzi watakatifu hawa wapya kwa maadhimisho ya: Ibada, Liturujia
pamoja na kuwaweka kuwa walinzi na wasimamizi wa shughuli mbali mbali katika maisha
na utume wa Kanisa. Itakumbukwa kwamba, Mtakatifu Yohane Paulo II atakuwa ni msimamizi
wa Siku za Vijana Duniani.