2014-04-30 08:47:03

Makardinali washauri wakuu kukamilisha kazi yao mwaka 2015


Mkutano wa Makardinali washauri wakuu wa Papa Francisko katika mchakato wa mageuzi ndani ya Kanisa kuanzia tarehe 28 hadi tarehe 30 Aprili 2014 wamekuwa na vikao ambavyo vinahudhuriwa pia na Baba Mtakatifu Francisko hapa mjini Vatican kadiri ya nafasi ya ratiba yake.

Hili ni kundi la Makardinali wanane walioteuliwa na Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni ili kumshauri katika masuala ya kufanya mabadiliko makubwa katika Sekretarieti ya Vatican kadiri ya matakwa yaliyooneshwa na Makardinali wakati wa mikutano yao elekezi kabla ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Mikutano hii pia inahudhuriwa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, ambaye kimsingi ndiye mtendaji mkuu katika Sekretarieti ya Vatican.

Hadi sasa Makardinali wamesikiliza kwa umakini mkubwa taarifa kutoka kwa Joseph F. X. Zahra, Rais wa Tume ya Kipapa inayojishughulisha na masuala ya uchumi na uongozi mjini Vatican, COSEA, mintarafu sekta ambazo zimechambuliwa na tume yake.

Makardinali wamepembua kwa kina na mapana Mabaraza ya Kipapa yanayotekeleza dhamana na utume wake mjini Vatican, kwa sasa wameanza uchambuzi wa Halmashauri za Kipapa na baadaye watafanya upembuzi wa jumla. Makardinali wataendelea na kazi yao tena kuanzia tarehe 1 hadi tarehe 4 Julai 2014.

Taarifa iliyotolewa na Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican inabainisha kwamba, bado kuna kazi kubwa inayoendelea kufanywa na Makardinali hawa na pengine, inaweza kukamilika ifikapo mwaka 2015. Ijumaa tarehe 2 Mei 2014 kutakuwa na mkutano wa kwanza wa Baraza la Kipapa la Uchumi.







All the contents on this site are copyrighted ©.