2014-04-30 10:11:00

Haki, amani na upatanisho ni mchakato unaohitaji ushirikiano wa dhati!


Askofu Gervas Nyaisonga aliyeteuliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki Mpanda anasema kwamba, rushwa inabomoa msingi wa haki na amani na kwamba, kuna haja kwa Kanisa kuendelea kushirikiana na wataalam, vyombo vya habari na serikali ili kufichua vitendo vya rushwa, ili hatimaye, kujenga utawala wa sheria, haki na amani. RealAudioMP3

Askofu Nyaisonga katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, Kanisa linahitaji kushirikiana na wadau mbali ili kujenga na kudumisha misingi ya ukwel, uwazi, uadilifu na uwajibikaji. Wataalam wafanye tafiti za uhakika ili kubainisha mianya ya rushwa, ili kuweza kujenga hoja ya nguvu katika mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi, vinginevyo, mapambano haya yanageukwa kuwa ni majungu.

Ili kuimarisha upatanisho na umoja wa kitaifa, Jamii inapaswa kujielekeza katika kujitambua na kujikubali, tayari kuanza mchakato wa pamoja katika kulinda na kudumisha mafao ya wengi badala ya kukumbatia misimamo binafsi au ya vikundi ambayo wakati mwingine inaweza kuwa na madhara makubwa katika Jamii.

Askofu Gervas Nyaisonga anasema, haki, amani na upatanisho ni mchakato unaohitaji ushirikiano na mshikamano na wadau mbali mbali, ili kujenga msingi wa umoja na mshikamano wa kitaifa, vinginevyo wananchi wanaweza kutawaliwa na hofu na wasi wasi zisizo na msingi.







All the contents on this site are copyrighted ©.