2014-04-29 07:21:26

Mchango wa Kanisa katika ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ghana


Askofu mkuu Jean Marie Speich, Balozi wa Vatican nchini Ghana, hivi karibuni aliwasili nchini Ghana na kupokelewa na viongozi wa Kanisa na Serikali nchini humo baadaye kuhudhuria hafla fupi ya “Akwaba” kadiri ya mapokeo ya wananchi wa Ghana. RealAudioMP3

Tarehe 27 Januari 2014 Askofu mkuu Speich aliwasilisha nakala za hati zake za utambulisho na kupokelewa na Naibu Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ghana, Bwana Kwesi Quartey. Viongozi hao wawili wamepongeza mchango wa Kanisa katika kuleta maendeleo kwa wananchi wa Ghana katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Serikali ya Ghana imepongeza ubora wa elimu na wainjilishaji wanaojitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi wa Kanisa na maendeleo ya watu wa Ghana. Serikali inampongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa unyofu na jitihada zake za kuwa ni sauti ya wanyonge na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Tarehe 28 Januari 2014, Askofu mkuu Jean Marie Speich aliwasilisha hati zake za utambulisho kwa Rais wa Ghana Bwana John Draman Mahama, baada ya kumkaribisha kwenye Ikulu ya Ghana. Rais amewashukuru na kulipongeza Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana kwa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu, utu na heshima ya binadamu bila kusahau ustawi na mafao ya wengi.

Askofu mkuu Jean Marie Speich amewasilisha salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa Rais na wananchi wa Ghana katika ujumla wao. Baba Mtakatifu ameipongeza Ghana kwa kumteuwa Balozi mkazi atakayeshughulikia masuala ya Ghana mjini Vatican.

Lengo ni kuendelea kushirikiana na wadau mbali mbali kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ghana kwa sasa na kwa siku za usoni. Askofu mkuu Speich anasema, uwepo wake nchini Ghana kama Balozi wa Vatican ni kuendeleza mchango wa Kanisa katika kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu pamoja na kujikita katika mchakato wa maendeleo na ustawi wa wananchi wote wa Ghana.

Tarehe 6 Februari 2014, Askofu mkuu Speich alikutana na viongozi wakuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana pamoja na kuwasilisha barua ya utambulisho kutoka kwa aliyekuwa Askofu mkuu Pietro Parolin, katibu mkuu wa Vatican ambaye hivi karibuni alisimikwa rasmi kuwa ni Kardinali. Baadaye Askofu mkuu Speich alitembelea Majimbo makuu yanayounda Kanisa Katoliki Ghana kwa kukutana na kuzungumza na Maaskofu wakuu pamoja na waamini wao.








All the contents on this site are copyrighted ©.