Kanisa Barani Afrika limefuatilia kwa umakini mkubwa ushuhuda wa maisha ya Mtakatifu
Yohane Paulo wa pili aliyesimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai dhidi ya
utamaduni wa kifo, unaosimikwa katika sera za utoaji mimba na kifo laini. Hizi ni
juhudi ambazo hazina budi kulindwa na kuendelezwa kama njia ya kuenzi mchango wa Mtakatifu
Yohane Paulo wa Pili katika kudumisha utu na heshima ya binadamu, aliyeumbwa kwa sura
na mfano wa Mungu.
Askofu Anthony Mukobo wa Jimbo Katoliki la Isiolo, Kenya
amekubali kimsingi wazo la kuipatia Hospitali ya wanawake na watoto Jimboni humo,
jina la Mtakatifu Yohane Paulo II. Hili ni wazo lililojitokeza kunako mwaka 2005 mara
tu baada ya kifo cha Papa Yohane Paulo II, aliyependwa na wengi, kutokana na mchango
wake katika kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu, si tu kwa maneno matupu,
bali kwa njia ya ushuhuda wa maisha yake. Ni kiongozi aliyepokea mateso na kuyapatia
maana mpya kwa kuimarisha imani na matumaini.
Hospitali ya Mtakatifu Yohane
Paulo II, inatoa huduma kwa Mama na Mtoto katika Jimbo la Isiolo, Kenya. Huduma hii
inapania pamoja na mambo mengine kupunguza vifo vya wanawake wajawazito na watoto
wenye umri chini ya miaka mitano. Kwa kuwa na usafiri wenye uhakika, wanawake wenye
matatizo ya kijufungua wanaweza kukimbizwa mara moja kwenye Hospitali kubwa ili kuokoa
maisha ya Mama na mtoto. Juhudi hizi hazina budi kwenda sambamba na maboresho ya miundo
mbinu, kwa kuwa na usafiri wenye uhakika na salama kwa wanawake wajawazito.
Hospitali
ya Mtakatifu Yohane Paulo II imeanza kuwa mstari wa mbele kwa kutoa huduma makini
kwa Mama na Mtoto vijijini sanjari na kuwaandaa wakunga wa jadi wanaosimamiwa na kupewa
mafunzo na wauguzi waliobobea, ili kuendelea kutoa huduma bora zaidi kwa wanawake
wajawazito vijijini. Inasikitisha kuona kwamba, wanawake wengi wanapoteza maisha wakati
wa kujifungua, hali ambayo inachangia ongezeko la vifo vya wanawake wajawazito na
watoto chini ya umri wa miaka mitano.
Takwimu zinaonesha kwamba, wanawake
wanaoishi katika Nchi zinazoendelea duniani wanapata mimba kwa wingi ikilinganishwa
na wanawake wanaoishi katika Nchi tajiri zaidi duniani, ambao wengi wao kwa sasa mambo
ya uzazi hayana tena msukumo wa pekee, bali wanataka kuponda mali na kuvinjari maisha.
Kuna haja ya kufanya maboresho ya huduma ya Mama na mwana kwenye kambi za wakimbizi,
kwa kutambua umuhimu wa wanawake katika kuchangia ustawi na maendeleo ya nchi zao.
Watetezi
wa haki msingi za wanawake wanasema, kuna haja kwa jamii kudhibiti vitendo vya unyanyasaji
na dhuluma dhidi ya wanawake kwa kuwapatia haki zao msingi pamoja na kuthamini utu
wao kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Wanawake wasaidiwe kiroho
na kimwili, ili waweze kutekeleza dhamana na utume wao ndani ya Jamii na Kanisa katika
ujumla wake. Wanawake wakiwezeshwa kwa njia ya elimu makini na uchhumi endelevu, wanaweza
kusaidia katika mchakato wa maboresho ya familia na jamii inayowazunguka.