2014-04-28 09:14:05

Wabudha na Wakristo wanahamasishwa kujenga udugu!


Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini katika maadhimisho ya Siku kuu ya Vasakh inayoadhimishwa na waamini wa dini ya Kibudha, kila mwaka ifikapo tarehe 6 Mei huko Asia Mashariki ambayo pia husherehekewa sehemu mbali mbali za dunia kati ya tarehe 13 na tarehe 14 Mei ya kila Mwaka. Kauli mbiu inayoongoza maadhimisho haya ni: “Wabudha na Wakristo kwa pamoja wajitahidi kujenga udugu”. RealAudioMP3

Ni kauli mbiu inayopata chimbuko lake kutoka kwenye ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya kuombea amani duniani kwa Mwaka 2014, aliyekazia kwamba, udugu ni msingi na njia ya amani. Udugu ni kigezo muhimu sana katika maisha ya mwanadamu kinachomwezesha mtu kumthamini na kumhudumia jirani yake kama binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Huu ni msingi wa ujenzi wa Jamii inayosimikwa katika msingi wa haki na amani ya kudumu.

Uhusiano wa kidini unaojengeka katika misingi ya urafiki, majadiliano, ukarimu na mapendo ya dhati ni mambo ambayo yanajenga na kuimarisha mahusiano ya kidugu. Mzizi mkuuwa fitina na chuki ni ujinga unaosababishwa na waamini kutofahamiana kwa dhati na kwamba ubinafsi umekuwa ni chanzo cha vita na uvunjifu mkubwa wa haki msingi za binadamu. Mambo haya yanasababisha watu kutoonana na kupendana, ili kujenga na kuimarisha umoja.

Wabudha na Wakristo wanaishi katika ulimwengu ambamo bado kuna dhuluma, ubinafsi, ukabila, kinzani za kikabila, vita, misimamo mikali ya kiimani, hali ya baadhi ya watu ndani ya Jamii kujisikia wanyonge au kuonekana kuwa ni tisihio na hivyo kuwa ni sababu ya kuondolewa kwao kutoka katika uso wa dunia. Waamini wanahamasishwa kushirikiana na watu wote wenye mapenzi mema, ili kuheshimu na kuendeleza msingi wa maisha ya binadamu katika medani mbali mbali za maisha.

Waamini kwa pamoja wanapaswa kusimama kidete kukemea dhambi za kijamii zinazoathiri udugu; kujitahidi kuwa ni wajenzi wa ukarimu na wadau wa upatanisho, wanaojitahidi kuvunja kuta za utengano ndani ya Jamii ili kujenga na kuimarisha Jamii inayosimikwa katika udugu kati ya mtu mmoja mmoja na makundi ya watu.

Duniani kuna mambo yanayowaunganisha watu katika utu na heshima yao kama binadamu na hivyo wanashiriki katika mchakato wa ujenzi wa dunia inayosimikwa katika haki, amani na udugu, jambo linalohitaji utambuzi wa pamoja wa tunu hizi msingi. Majadiliano ya kidini ni njia muafaka ya kutambua na kuenzi tunu hizi zinazojikita katika maadili, ili kujenga umoja na udugu kama sehemu ya Familia ya binadamu.

Kila mwamini anachangamotishwa kuwa ni mjenzi wa amani kwa kukataa katu katu sera za chuki, ili kujenga ulimwengu unaojikita katika utamaduni wa majadiliano na kukutana na watu. Juhudi hizi hazina budi kujikita katika malezi, hasa miongoni mwa vijana wa kizazi kipya, ili waweze kuwa na ujasiri wa kujenga udugu. Baraza la Kipapa linahitimisha ujumbe wake kwa waamini wa dini ya Budha kwa kuwatakia Siku kuu njema ya Vasakh, ili kweli iwe ni fursa ya kuendeleza udugu katika Jamii ambazo bado zimegawanyika. Ujumbe huu umetiwa sahihi na Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya kidini.








All the contents on this site are copyrighted ©.