Kardinali Stanislaw Dziwisz, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Krakovia, Poland katika Ibada
ya shukrani iliyofanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican
Jumatatu tarehe 28 Aprili 2014 anamshukuru Mungu kwa kumwezesha Mtakatifu Yohane Paulo
II, Baba wa huruma ya Mungu, kutekeleza kwa dhati kabisa mafundisho ya Mtaguso mkuu
wa Pili wa Vatican pamoja na kuliandaa Kanisa kuingia katika Millenia ya tatu ya Ukristo.
Kardinali Dziwisz anasema, shukrani hizi ni kutokana na ushuhuda angavu na
wa kweli unaojikita katika upendo na huduma kwa wote, kama walivyoonesha watakatifu
hawa wapya katika maisha na utume wao kama viongozi wakuu wa Kanisa. Waamini wanamshukuru
Baba Mtakatifu Francisko kwa kuridhia ombi la kuwatangaza Mapapa hawa wawili kuwa
Watakatifu, mchakato ambao ulianzishwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, tukio
muhimu sana kwa ajili ya Kanisa zima.