Mtakatifu Yohane Paulo II alitetea Injili ya Familia, Uhai na akaonesha Ibada kwa
Bikira Maria
Miaka tisa imekwisha yoyoma tangu Yohane Paulo II alipofariki dunia, umati mkubwa
wa Familia ya Mungu, ukashuhudia jinsi ambavyo, Yohane Paulo II alivyokuwa mtii katika
Injili ya Kristo, kiasi kwamba, alijitosa bila ya kujibakiza ili kuitolea ushuhuda
Injili ambayo ni mwanga na matumaini kwa Wakristo wa vizazi vyote.
Mama Kanisa
ametambua utakatifu wa Yohane Paulo II, changamoto na mwaliko wa kujitahidi kutoa
mfano wa maisha yake kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Ni kiongozi aliyethubutu
kuwatangazia walimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yake uwepo wa Kristo kati ya
watu wake. Aliwainjilisha watu kwa njia ya mateso na mahangaiko yake, akawaonjesha
imani thabiti inayojikita katika Fumbo la Msalaba, kiasi kwamba, imani yake ikang'aa
katika giza na wasi wasi wa maisha ya watu!
Ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa
na Kardinali Angelo Comastri katika Ibada ya Misa takatifu kwa ajili ya kumshukuru
Mungu kwa Mama Kanisa kuwatangaza watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuwa
Watakatifu. Ibada hii imeadhimishwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro
mjini Vatican, Jumatatu, tarehe 28 Aprili 2014.
Mtakatifu Yohane Paulo II
alisimama kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya kifamilia dhidi ya sera
na mikakati iliyokuwa inalenga kubomoa taasisi ya familia. Mama Kanisa anatambua umuhimu
wa familia katika Jamii, ndiyo maana anaendelea kutangaza ukuu wa maisha ya ndoa na
familia kadiri ya mpango wa Mungu.
Mtakatifu Yohane Paulo II anasema kwamba,
Familia ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, inapaswa kulindwa na kudumishwa
hata kama ni kwa kujisadaka kwa njia ya maisha, kama ilivyotokea kwake, ili walimwengu
waweze kusoma na kuitafakari Injili ya mateso ya familia, kama maandalizi makini ya
kulinda na kuitetea familia katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Mtakatifu
Yohane Paulo II alisimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai, dhidi ya utamaduni
wa kifo unaokumbatia sera za utoaji mimba, ubinafsi na hali ya kutojali wala kuguswa
na utakatifu wa maisha. Mtakatifu Yohane Paulo II alikuwa na Ibada kubwa kwa Bikira
Maria Mama wa Mungu na Kanisa, ndiyo maana alipenda kumkabidhi Injili ya Uhai, ili
aweze kusaidia kulinda na kuwaombea watu waliokuwa wanateseka kwa kutolewa mimba,
vita, dhuluma na nyanyaso dhidi ya wasichana na wanawake pamoja na kifo laini.
Mtakatifu
Yohane Paulo II alikemea vita kwa nguvu zote kwa kuwakumbusha wakuu wa Jumuiya ya
Kimataifa kwamba, vita inasababisha mateso na majanga katika maisha ya watu wengi
na kamwe haiwezi kuleta suluhu ya matatizo yanayojitokeza katika uso wa dunia. Hizi
ni dalili za binadamu kutembea katika utupu, mwaliko kwa waamini na watu wote wenye
mapenzi mema, kumkimbilia Yesu Kristo ili aweze kuwapatia utimilifu wa maisha.
Vijana
kutoka sehemu mbali mbali za dunia, walimtambua Mtakatifu Yohane Paulo II kama Baba,
rafiki na mlezi. Alionesha, uaminifu, furaha na ukamilifu wa maisha na utume wa Kipadre
wakati wa kinzani na utepetevu wa maisha na maadili ya Kipadre kwa kujitoa bila ya
kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Kwa hakika aliwasaidia waamini wengi
kujenga na kukuza Ibada kwa Bikira Maria baada ya mtikisiko uliosababishwa na Mtaguso
mkuu wa Pili wa Vatican.
Mtakatifu Yohane Paulo II anatambua kwamba, ni kwa
msaada na ulinzi wa Bikira Maria aliweza kunusurika na kifo siku ile ya tarehe 13
Mei 1981, akajiweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria kwa maneno haya "Totus
tuus". Kwa ufupi anasema Kardinali Angelo Comastri, huyu ndiye Mtakatifu Yohane Paulo
II