2014-04-28 09:44:47

Mnaitwa kuwa watakatifu!


Mpendwa Msikikizaji wa Radio Vatikani, karibu kwa mara nyingine tena katika kipindi chetu cha Kanisa la Nyumbani. Tunaendelea kuungana na Mama Kanisa kumshukuru Mungu kwa zawadi ya Watakatifu Yohane Paulo II na Yohane wa XXIII, walioandikwa karika Orodha ya Watakatifu na kutangazwa rasmi katika Dominika ya Huruma ya Mungu. RealAudioMP3

Ni neema ya pekee mpendwa msikilizaji, kushuhudia watu hawa walioishi nyakati zetu, waliotugusa kwa maadhimisho ya neno na Sakramenti kama makuhani wa Bwana, na zaidi walioliongoza Kanisa la Mungu katika hija yake hapa duniani. Hivyo tumeshuhudia maisha yao, wito wao, kazi na jasho lao, na tulishuhudia jinsi walivyompendeza Mungu na zaidi sana tunashuhudia jinsi wanavyoandikwa katika orodha ya watakatifu.

Ni heri kubwa kwetu kushuhudia mambo haya. Basi nasi tukijawa hamu ya kushiriki karamu ya wateule mwisho wa uzima huu, tunahimizwa, tunatiwa moyo kwa mfano wa maisha yao. Na katika hili tunazidi kuaminishwa ya kwamba, utakatifu inawezekana. Neno la Mungu linatualika sote, likisema “Wakumbukeni viongozi wenu waliowahubirieni Neno la Mungu. Fikirini juu ya mwenendo wao, mkaiige imani yao”. Hebr. 13:7

Katika kipindi hiki tutafakari kwa uchache juu ya wito wa kuwa mtakatifu. Kwa mwangwi wa mafundisho ya Kanisa, sisi sote tumeitwa kuwa watakatifu (Rejea Sheria ya Kanisa, na 210, Hati ya Mtaguso – Mwanga wa Mataifa nn 39-40). Utakatifu sio kitu ambacho mtu hupewa baada ya kufa, hapana. Utakatifu ni hali nzima ya maisha ambayo mtu hujibidisha kuitafuta na kuiishi duniani hapa na mwisho kushirikishwa uzima ule wa milele mbinguni.

Sisi tulio hai, tumeitwa kuwa watakatifu na pia tunatamani, mwisho wa maisha yetu haya, tukaunganika na Kanisa la Watakatifu huko mbinguni. Tuwapo hapa duniani, tunasafiri (ndiyo maana tunaitwa Kanisa linalohiji), tunapigana vita vya kiroho na kimwili. Na kwa msaada wa Neno la Mungu, Sakramenti, sala, Ibada, Liturujia, matendo ya upendo kwa Mungu na jirani, tunatazamia mwisho ule mwema, yaani muungano kamili na Mungu aliye lengo-kikomo letu. Mwisho wa jitihada zote tunatamani tukamwone Mungu, tukaishi naye milele.

Watakatifu ni nani? Ni watu ambao, walipokuwa hapa duniani walimpendeza Mungu kwa maisha yao. Walijibidisha kumjua Mungu wa kweli, kumpenda na kumtumikia. Na baada ya kuondoka kwao katika uzima huu, Mungu ameendelea kutenda kazi ndani mwao na kwa njia yao, kwa ishara na miujiza mbalimbali, inayodhihirisha nguvu hiyo ya Mungu. Kwa sababu ya maisha yao na ishara hizo, Mama Kanisa Mtakatifu, kwa uongozi wa Mungu mwenyewe, anawaandika rasmi katika orodha ya Watakatifu.

Kumtangaza mtu kuwa mtakatifu ni MCHAKATO. Mchakato huu unaongozwa na Imani Takatifu, taratibu-kanuni za jumla na za kipekee. Mama Kanisa anazo taratibu maalumu za kufuata hata mtu aliyeitwa kutoka dunia hii, aweze kutangazwa kuwa mtakatifu. Tunapotafakari juu ya zawadi ya watakatifu wetu wapya, tujulishane kwa ufupi hatua zinazofuatwa hadi mtu aweze kutangazwa kuwa mtakatifu.

Baada ya kufariki mtu, na kisha kuona baadhi ya ishara na miujiza, inayosindikizwa na aina ya maisha ambayo huyo mtu aliishi na aina ya kifo alichokufa, kisha kupita miaka mitano baada ya kufariki, ndipo wahusika huweza kuanza kuomba ruhusa kutoka kiti kitakatifu ya kuanza mchakato wa kumtangaza mtu kuwa ni mtakatifu. Ruhusa hiyo huweza kuombwa na wanandugu au kundi la waamini, au shirika la kitawa kama alikuwa mtawa. Ruhusa hiyo inaombwa kupitia kwa askofu Jimbo, kule alikoishi au kufia mtu huyo. Kiti kitakatifu kikishakutoa ruhusa kwamba mchakato uendelee, basi kwa uruhusisho huo huyo aliyefariki haitwi tena marehemu, bali ni MTUMISHI WA MUNGU.

Baada ya uruhusisho huo, kamati maalumu ya watu wenye imani thabiti na wenye kujua thamani ya ukweli mbele ya Mungu, huanza kukusanya ushahidi juu ya maisha ya MTUMISHI WA MUNGU. Hapa kuna ushahidi wa maandishi kama aliyaacha, maneno aliyokuwa anatamka (masimulizi kutoka kwa watu), matendo yake ya kiimani kama vile maisha ya sala, sadaka na majitoleo; matendo yake ya upendo kwa jirani. Hayo yote hukusanywa na kuhakikiwa na ile kamati maalumu ngazi ya jimbo. Nayo huwakilisha uhakiki wao tena kwa Askofu Jimbo. Askofu jimbo ndiye mwenye wajibu msingi wa kuwaongoza waamini wake kwa Mungu.

Kisha hakikiwa na Askofu Jimbo, taarifa zote za MTUMISHI WA MUNGU hupelekwa tena katika Kiti Kitakatifu (katika ofisi maalumu inayohusika na kuwatangaza Watakatifu). Nako huko taarifa hizo huhakikiwa kwa Kanuni maalumu zinazoongozwa na Imani kwa Mungu na Kanisa lake katika Kristo Yesu. Taarifa hiyo ikiwa haina mawaa, hupelekwa kwa Baba Mtakatifu, naye kwa uwezo wa kimungu kama Wakili wa Kristo na kwa mamlaka aliyo nayo, huhukumu uhalali wa taarifa ya mtumishi wa mungu. Endapo taarifa hiyo itakuwa ni matendo mema ya ushuhuda na ushujaa wa imani, basi Baba Mtakatifu ataidhinisha huyo MTUMISHI WA MUNGU awe MHESHIMIKA. Na hivyo kanisa mahalia huweza kuanza tu kumheshimu.

Huyo MTUMISHI MHESHIMIKA WA MUNGU, akitenda walao muujiza mmoja, muujiza huo huhakikiwa na kamati ya Imani na WANASAYANSI, ili kuhukumu kuwa kweli ni muujiza, ni nguvu ya mungu imetendeka, iwe katika uponyaji au jambo lolote. Muujiza huo hudhihiridha nguvu ya Mungu inayotenda kazi kwa njia ya MTUMISHI MHESHIMIKA WA MUNGU. Taarifa hiyo ya Muujiza, hupelekwa tena katika kiti kitakatifu. Kiti kitakatifu kikiridhia uhalali wa muujiza au miujiza hiyo, hupeleka taarifa yote kwa Baba Mtakatifu. Na Baba Mtakatifu naye kwa nguvu ya kimungu na uwezo aliopewa, huhukumu na kumtangaza mtumishi wa mungu kuwa mwenyeheri.

Baada ya hapo, mchakato unaendelea wa kumtangaza MWENYEHERI kuwa Mtakatifu. Hapo ndipo huhitajika muujiza mwingine tena. Hadi hapo Kiti kitakatifu huweza kuruhusu Makanisa, Mashule na majengo mbalimbali kujengwa kwa heshima ya mwenye heri huyo, na huku watu wakiendelea kuomba msaada wa sala na maombezi yake. Ukiongezeka muujiza mwingine tena, na ukahakikiwa kwa mtindo uleule, hapo sasa mwenyeheri hutangazwa kuwa ni mtakatifu. Hivyo baada ya kufa tuna hatua hizi: MTUMISHI WA MUNGU, MHESHIMIKA, MWENYE HERI na mwisho MTAKATIFU. Hawa waliotangazwa Jumapili ya huruma ya Mungu, tarehe 27 Aprili 2014 WAMEPITIA HATUA HIZO ZOTE.

Kutangazwa kuwa mtakatifu ni tendo la kiimani na kiibada, linalofanywa na BABA MTAKATIFU, tendo ambalo kwa asili na kwa uvuvio wa Roho Mtakatifu, LIMEKINGWA NA KILA DOSARI, yaani KANISA KWA NJIA YA WATUMISHI WAKE, haliwezi kumtangaza Mtakatifu mtu asiyestahili. Na kisha kutangazwa Mtakatifu sasa, huyo hupewa tarehe maalumu ya kukumbukwa na Kanisa la Jumla, jina lake huandikwa katika orodho ya watakatifu na waamini huwalikwa kumfanya awe mwombezi na mfano wa maisha yake kuwa kielelezo cha maisha yetu ya kumtafuta Mungu.

Tunamwomba Mungu, kwa Maombezi ya Watakatifu Yohane wa XXIII na Yohane Paulo wa Pili, tujaliwe hali njema, tusafiri salama ili mwisho wa uzima huu, nasi tukamwone Mungu wetu. Kutoka Studio za Radio Vatican, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.