2014-04-27 09:41:18

Jibidisheni zaidi kugundua utajiri unaofumbatwa katika Nyaraka za Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican


Padre Raymond Saba, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican wakati huu Mama Kanisa anapomwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa kuwatangaza Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuwa watakatifu anasema, Yohane wa XXIII atakumbukwa sana na Kanisa Barani Afrika, lakini na Tanzania kwa namna ya pekee. Ni Papa aliyemteua Askofu Laurian Rugambwa kuwa Kardinali wa kwanza mwafrika, matendo makuu ya Mungu! RealAudioMP3

Wakati Tanganyika inajiandaa kupata uhuru wake, Papa Yohane XXIII alimzawadia Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Biblia ambayo hadi sasa inatunzwa Seminari kuu ya Kipalapala, Jimbo kuu la Tabora, ili iweze kusaidia katika kuaongoza watanganyika kwa wakati huo, kwa hekima, busara na kweli za Kiinjili. Leo hii, Jimbo Katoliki la Musoma, liko katika mchakato wa kumtangaza Mtumishi wa Mungu Mwalimu Nyerere kuwa ni Mwenyeheri, kutokana na mfano bora wa maisha kama mwamini mlei na mwanasiasa mahiri duniani.

Papa Yohane XXIII ndiye aliyetunga Sala maalum kwa ajili ya kuiombea Tanzania na watu wake, ili iweze kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa dhati. Tanzania anasema Padre Saba imezaliwa na kulelewa katika fukuto la maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Maaskofu wazalendo saba kutoka Tanzania walihudhuria maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican yaliyokuwa yameitishwa na Papa Yohane XXIII.

Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ni chombo makini na dira rejea katika maisha na utume wa Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Changamoto ambayo bado iko mbele ya Familia ya Mungu ni kuendelea kujifunza kwa bidii zaidi Mafundisho ya Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ili kugundua tena na tena utajiri unaofumbatwa katika Nyaraka hizi.







All the contents on this site are copyrighted ©.