2014-04-25 09:58:45

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Pili ya Pasaka, maarufu kama Jumapili ya Huruma ya Mungu!


Tunaendelea tena katika tafakari yetu masomo Dominika ya II ya Pasaka mwaka A. Ni kipindi cha furaha kwa sababu ya ushindi dhidi ya kifo kwa njia ya ufufuko. Neno la Mungu, linakazia na kuahidi furaha ya kweli kwa wale ambao hata kama hawakumwona Bwana wanayo imani na tumaini la kweli katika yeye. RealAudioMP3

Katika Somo la kwanza, kutoka katika kitabu cha Matendo ya Mitume latuonesha furaha na tabia ya jumuiya ya kwanza ya Yerusalemu. Kwa nini tunaoneshwa jambo hilo? Ni kwa sababu tunaalikwa kuishi mtindo uleule wa jumuiya ya mwanzo katika mazingira yetu. Mambo msingi ya Jumuiya ya I yalikuwa utii na usikivu wa watu kwa Neno la Mungu lililohubiriwa na Mitume. Aidha waliweka mali yao na moyo wao pamoja kwa faida yao na kasi ya Injili.

Ili kuimarisha mambo haya waliadhimisha pamoja Ekaristi Takatifu na kusali pamoja kwa upendo. Mambo haya msingi yalifungamana na furaha, uchangamfu, ushirikiano ambavyo vilikuwa vivutio kwa jumuiya nyingine nje ya Yerusalemu. Ndiyo kusema waliishi na kukishuhudia kile walichohubiri katika maisha yao, yaani waliuishi ufufuko ambao ndilo chimbuko la haya yote.

Mpendwa msikilizaji, wito kwetu hivi leo katika jumuiya zetu ni kuanza polepole kupalilia nguvu ya ufufuko, ndiyo kusema tunaalikwa kushuhudia daima kwa maisha yetu yakuwa Kristu ni mfufuka. Mpendwa, katika mantiki hiyo katika jumuiya zetu lazima tabia za jumuiya ya kwanza zijitokeze na kukua na hivi kuwa kielelezo cha mapendo kwa watu wa mataifa. Yafaa kukomaza ile tabia ya kushirikishana tulichonacho hata kama ni kidogo. Tujifunze kuwa na kile kinachotufaa na kinachobaki kiwe kwa ajili ya wale waliowahitaji katika jumuiya zetu.

Kumbuka usemi wa Mtakatifu Basil akisema “kama mmoja wetu angechukua kwa ajili yake kinachohitajika na kingine kikawa kwa ajili ya ndugu yake maskini, basi kusingekuwa na tajiri wala maskini katika jumuiya”. Hii ni falsafa ya mgawanyo sawa ambayo tungepaswa kuifikia kama kweli tunataka kumfuasa Bwana kwa ukamilifu! Mpendwa msikilizaji inaonekana kuna ugumu katika kushirikishana mali tulizonazo, na hasa kuwapeni maskini, je toka tukiamini na kuendelea katika ugumu huu twaweza kusema tunaishi na tunashuhudia ufufuko? Tafakari sana jambo hili!

Katika somo la Pili toka barua ya kwanza ya Mtakatifu Petro tunakumbushwa siku ya ubatizo wetu. Kwa njia ya ubatizo tulipata kuingia katika furaha isiyo na mwisho. Ndiyo kusema Mt Petro anataka hata kama kuna madhulumu na taabu mbalimbali tusisahau furaha ya milele. Anasema mateso ni ya kitambo kidogo tu na baadaye yanapita cha msingi ni kutazama mbele tukiendelea kukua katika neema ya ubatizo.

Mtakatifu Petro anatukumbusha kuwa mkristu katika ulimwengu huu ni mgeni na hivi yuko safarini kwenda nchi ya ahadi yaani mbinguni. Tunakumbushwa kuwa hakuna mateso yanayoweza kuzima moto wa furaha na mapendo uliowashwa wakati wa ubatizo. Wakristo ni kama dhahabu ambayo ili itengeneze kitu cha thamani lazima ipitie moto ili ichomwe na kusafishwa tayari kwa kito cha thamani.
Katika somo la Injili, hali ya maisha ya jumuiya inajionesha wazi. Wanafunzi wako pamoja ingawa wanahofu! Bwana anawakuta wakiwa pamoja na kuwatakieni amani. Anawaonesha alama za madonda na wanafurahi na kusema tumemwona Bwana! Ni katika jumuiya hiyo Bwana anawavuvia Roho Mtakatifu ili wapate kuondolea dhambi. Ni siku hii anaweka sakramenti ya kitubio katika Kanisa na kisha anawatuma wakaende kutangaza habari njema. Kumbe Toba ni mlango wa kazi ya kimisionari, ni mlango wa imani, ni mlango wa wokovu. Analikabidhi kanisa ufunguo wa kufunga na kufungua katika mambo yamhusuyo Mungu katika uhusiano wake na mwanadamu.
Jumuiya wakati fulani zinakuwa na watu walio na mashaka katika imani. Hali hii inajionesha leo pia. Ndiyo kusema, kumbe Mtume Tomaso ambaye hakuwapo pamoja na wenzake siku ya kwanza haamini, bado ana mashaka kuhusu ufufuko! “Siamini mpaka nitie vidole vyangu katika makovu ya Bwana! Baada ya siku nane tukio hilo la kitaalimungu, Bwana anawatokea tena Mitume na wakati huo Tomaso yupo.
Bwana anamwambia lete mikono yako na uweke kidole chako katika ubavu wangu na usiwe asiyeamini! Tomaso anajibu, Bwana wangu na Mungu wangu! Mpendwa, Mtume Tomaso anapokiri udhaifu wake anatufundisha kuwa watu wa Imani na unyenyekevu mkubwa na hivi baada ya ufufuko hakuna mashaka tena kinachobaki ni kwenda kutangaza habari ya furaha kwa mataifa.
Mpendwa leo hii wapo watu wa namna hii katika jumuiya zetu, kumbe wanaalikwa na Bwana kusadiki pasipo kuona, na kwa namna hiyo Bwana anatangaza heri kwa wasioona wakasadiki na si kwa wanaosadiki kwa sababu ya kuona. Mwishoni mwa sehemu ya Injili ya Dominika hii, Mwinjili anatuambia pia zipo ishara nyingi ambazo hazikuandikwa na hivi mtu asishangae ishara nyingine ambazo hazimo katika Biblia lakini ni muhimu kwa imani yetu na maisha ya Kanisa.
Nakutakieni furaha tele katika kipindi chote cha Pasaka na Mungu azidi kuwa nawe, nawe ukitekeleza mapenzi yake katika Jumuiya kama Jumuiya ya kwanza ya Waamini. Tukutane tena Dominika ijayo. Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.