2014-04-24 11:16:29

Viongozi wa Kanisa wanalaani mauaji ya watu wasiokuwa na hatia!


Askofu mkuu Dieudonnè Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati amelaani mauaji ya Padre Christ Forman Wilibona kutoka Jimbo la Bossangoa aliyeuwawa kikatili katika maadhimisho ya Ijumaa kuu. Viongozi wa Kanisa wanawaalika waamini na wananchi wote wenye mapenzi mema kuungana kwa pamoja ili kuombea amani na utulivu nchini humo sanjari na kuendelea kujikita katika majadiliano yanayolenga kudumisha mchakato wa haki, amani na upatanisho wa kitaifa.

Mauaji ya Padre Christ Forman Wilibona yametokea siku chache tu baada ya kikundi cha Seleka kumteka Askofu mkuu Nestor-Dèsirè Nongo Aziagbya wa Jimbo kuu la Bossangoa pamoja na Mapadre watatu. Katika siku za hivi karibuni kumekuwepo na ongezeko la vitendo vya mauaji ya kutisha Kaskazini Mashariki mwa Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati.

Viongozi wa Kanisa wanawataka wananchi wa Afrika ya kati kuondokana na mauaji ya watu wasiokuwa na hatia na kuanza kujikita katika mchakato wa upatanisho wa kitaifa. Wanatoa mwaliko pia kwa Jumuiya ya Kimataifa kusaidia harakati za kurudisha tena utawala wa sheria pamoja na kuwapokonya wana mgambo silaha, kwani wamekuwa ni chanzo cha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia.







All the contents on this site are copyrighted ©.