Ninakuleteeni furaha ya Pasaka kwa njia ya tafakari ya Neno la Mungu. Ni Vijilia ya
Pasaka, yaani, Jumamosi kuu. Ni kesha la usiku mtakatifu ambapo Kristu mshindaji amejipatia
taji kwa kuyashinda mauti.
Ni siku
ambayo Kristu hayumo tena kaburini bali yu mzima na kwa maana hiyo, Kanisa popote
duniani linashangilia na kuimba aleluya. Katika litrujia ya usiku mtakatifu, Kanisa
laelezea jinsi ambavyo Kristu ni Nuru, linaimba sifa za nuru hii kwa njia ya Mbiu
ya Pasaka. Kanisa linashangilia ushindi toka upotevu wa mwanadamu na kuelekea uhuru
kamili unaoletwa na Kristu mfufuka.
Liturujia ya Jumamosi Kuu imegawanyika
katika sehemu kuu nne, yaani litrujia ya Mwanga, litrujia ya Neno, liturujia ya Ubatizo
na litrujia ya Ekaristi Takatifu. Katika sehemu hizi kuu nne Mama Kanisa ataka tuelewe
polepole jinsi ukombozi ulivyotufikia kwa njia ya Masiha.
Katika Liturujia
ya Mwanga kawaida tunaanza na ishara ya moto ambao huleta joto na mwanga, hufukuza
baridi na giza. Moto unaowaka huonesha uwepo wa Mungu katikati yetu. Alama hii tunaiona
pale Wana wa Israeli walipokuwa wakitoka Misri waliongozwa na moto katika wingu. Katika
Agano Jipya tunaona ndimi na miali ya moto siku ya Pentekoste na hivi Roho Mtakatifu
alitua kwa kila mmoja wa Mitume waliokuwa pamoja na Bikira Maria. Moto ni alama ya
utakaso toka uovu na kuelekea utakatifu au wajibu wa kitume, hebu kumbukeni jinsi
Nabii Isaya alivyowekewa kaa la moto kinywani mwake na hivi akatangaziwa utakaso wa
roho, tayari kwa kazi ya kinabii ( Isa. 6:6-7).
Katika Liturujia ya Kanisa
kwa sasa, moto ubarikiwa ili uwe ishara ya upendo na maelewano katika familia, ishara
ya kufukuza giza yaani shetani katika maisha ya kikristu. Kumbe tunapowasha Mshumaa
wa Pasaka na mishumaa yetu mingine toka moto huu tunataka kumwahidi Bwana zawadi nzuri
ya upendo, utayari, heshima tutakayomrudishia sisi wenyewe. Kwa ujumla mshumaa ni
uwepo wa Mungu katikati ya mataifa, katikati yetu na tunasema ni Mungu milele. Angalia
taa ya milele kanisani ashilio la uwepo wa Mungu katika Ekaristi takatifu, daima katikati
yetu.
Maandamano toka moto wa Pasaka hadi kuimbwa Mbiu ya Pasaka SIFA KWA
MSHUMAA ishara ya Kristu humaanisha kuwa Kanisa linatoa sifa kwa Mwanga Mtakatifu
ndiye Kristu mfufuka. Mshumaa wa Pasaka katika Liturujia ya ubatizo utatumbukizwa
mara tatu, iliyo ishara ya Utatu Mtakatifu kwa maana ya kuyaweka wakfu maji katika
Utatu Mtakatifu na kwa njia hiyo, mwovu hufukuzwa ili watakaobatizwa katika kisima
hicho wapate nguvu ya Utatu Mtakatifu.
Mpendwa mwanapasaka, baada ya liturujia
ya mwanga huanza litrujia ya Neno la Mungu ambamo kanisa hutafakari historia ya mwanadamu
tangu kuumbwa kwake hadi anapokuja mkombozi na kumalizia kwa ufufuko kilele cha mapendo
ya Mungu kwa mwanadamu. Katika somo la kwanza tunaona Mungu anaumba kila kitu na anaona
ni chema kabisa. Kisha mama Kanisa anatuwekea mbele yetu Ibrahimu Baba wa imani katika
somo la pili. Matunda ya imani ya Ibrahimu ni uzao, baraka tele na wokovu. Mwaliko
kwetu ni kumsifu Mungu kwa kutuumba na kuomba kujaliwa imani kama ya Ibrahimu.
Katika somo la tatu kutoka katika kitabu cha Kutoka, tunapata kugundua maongozi
ya Mungu na upendo wake kwa wanadamu. Anawatoa Misri na anawavusha bahari na mto ishara
ya ubatizo, yaani kuzamishwa na kuibuka kuelekea ng’ambo ya pili ulioushindi na utakatifu.
Katika somo la Waraka kwa Warumi ujumbe mahsusi ni kuwa, kuishi kwetu ni Kristu,
kwa maana tulikufa naye katika mauti na kufufuka naye katika ubatizo. Sasa tuko wapya
na hivi mwaliko ni kuacha dhambi na kuendelea na maisha mapya.
Katika Injili,
habari ya ufufuko na ushindi dhidi ya mauti ndiyo imetanda na kupamba kila aina ya
adhimisho la Pasaka. Tunaona akina mama ambao Bwana ameamua kuwatuza wao kwanza zawadi
ya ufufuko ikiwa pia ni ishara ya kuinuliwa kwao toka ukiritimba wa kiyahudi na mfumo
dume uliokithiri. Wanaenda kaburini alfajiri na mapema. Wakiwa na mashaka juu ya nani
atawaondolea jiwe juu ya kaburi, wanakuta jiwe halipo juu ya kaburi bali limeviringishwa
pembeni na limekaliwa na kijana mwenye mavazi meupe! Jiwe ni alama ya kandamizo na
hivi kutokuwepo ni kwamba Bwana ni mshindi amelitupilia mbali kandamizo hilo linalowakilishwa
na jiwe! Walikuwepo walinzi, nao wanashangaa kilichotokea. Walinzi wanawakilisha mwovu
wakati akina mama wanawakilisha wakristu wenye furaha wanaoshangilia ushindi wa Masiha,
(Bwana ni mshindi, maisha yameshinda kifo).
Wanamwona kijana mwenye mavazi
meupe na anawapa taarifa kuwa Bwana hayupo amefufuka kumbe waende wakaseme kwa wanafunzi
wake kuwa awatangulia Galilaya kama alivyokuwa amewaambia. Kijana mwenye vazi jeupe
ni alama ya malaika anayetangaza kuwa Kristu ni wa juu na hivi ni mtakatifu na mzima.
Taarifa ya kwamba nendeni Galilaya ina maana kubwa sana, ya kwamba wasibaki alipofia
bali wafikirie ufufuko na wakaende kwenye jumuiya ya watu si kaburini. Ni mwanzo wa
umisionari, ni mwanzo wa msingi wa maisha ya mapendo ya kichungaji kwa jumuiya ya
watu.
Neno la Mungu ni taa ya kutuongoza na daima kama tangazo la imani
huita na kuzaa matunda ndiyo ubatizo. Kumbe baada ya litrujia ya Neno hufuata litrujia
ya ubatizo ambamo Mama Kanisa hupata watoto wapya. Kisima cha ubatizo hubarikiwa kwa
mshumaa wa pasaka na hivi nguvu ya Utatu Mtakatifu kwa ajili ya wabatizwa huwekwa
na Kristu mwenyewe aliye nuru na mwanga kwa wote. Kisima cha ubatizo hugeuka kuwa
tumbo la uzazi kama mama, huzaa watoto taifa teule la kikuhani, kifalme na kinabii.
Kwa njia ya ubatizo mtu huifia dhambi na kuacha mambo ya kale na kuingia maisha mapya.
Ubatizo ni kielelezo msingi na hasa ndiyo ufufuko. Wale waliokwisha batizwa zamani
wanaalikwa katika litrujia ya ubatizo kurudia ahadi zao za ubatizo na kusonga mbele
katika ufufuko. Na kwa jinsi hiyo kanisa linakua.
Mwishoni, mama kanisa
huadhimisha litrujia ya Ekaristi takatifu ambamo sasa waamini wapya hushirikishwa
kwanza ukamilifu wa Sakramenti za kuingizwa katika ukristu. Hushiriki meza ya mapendo
ya Kristu kwa mwanadamu. Hujipatia uzima wa milele kama tufahamuvyo toka Injili, ya
kuwa “aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu ataishi milele”. Waamini wote hushiriki
matunda ya pasaka Ekaristi Takatifu. Ni sadaka ya Kristu msalabani iliyo hai katika
ufufuko. Ekaristi ni umoja na chimbuko la umoja wa Kanisa na hivi wote waliofamilia
moja wanashiriki mkate mmoja wa mbinguni.
Mpendwa, nikutakieni heri na baraka
tele za Mungu katika sherehe za pasaka ukakirimiwe yote mema sasa na daima na milele.
Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.