2014-04-15 09:17:57

Biashara haramu ya binadamu inadhalilisha utu na heshima ya binadamu!


Wajumbe wa Baraza la Makanisa Duniani hivi karibuni walihabarishwa kuhusu ongezeko la biashara haramu ya binadamu duniani hali ambayo ni ukiukwaji mkubwa wa haki msingi, utu na heshima ya binadamu. Juhudi za kupambana na biashara haramu ya binadamu bado hazijazaa matunda yanayokusudiwa na Jumuiya ya Kimataifa. Hii ni changamoto kwa viongozi wa Makanisa kushirikiana kwa karibu zaidi na Serikali pamoja na vyama vya kiraia ili kuzuia na kukomesha kabisa biashara hii ambalo kwa sasa ni janga la kimataifa.

Hayo yamebainishwa na Joy Ngozi Ezeilo, mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu wakati alipokuwa anazungumza na wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni kuhusu masuala ya kimataifa na kwa namna ya pekee tatizo la uhamiaji na utumwa mamboleo.

Biashara haramu ya binadamu ni vitendo vya jinai vinavyojikita hasa katika biashara ya viungo vya binadamu, utalii wa ngono pamoja na hitaji la nguvu kazi kwa bei nafuu ili kuzalisha faida kubwa zaidi. Wajumbe wa mkutano huu, kwa kauli moja walisema kwamba, kuna haja kwa Viongozi wa Makanisa kusimama kidete kushughulikia tatizo hili linalodhalilisha utu na heshima ya binadamu, kwa kushirikiana na Serikali, Vyama vya kiraia pamoja na Umoja wa Mataifa.

Biashara haramu ya binadamu nchini Nigeria imejionesha kwa namna ya pekee kwa wizi wa watoto wadogo kutoka Hospitalini, Nyumba za kutunza watoto yatima pamoja na Kliniki, ambako baadhi ya wanawake kutokana na umaskini na uelewa kidogo wamejikuta "wakitapeliwa na kuingizwa mijini". Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kusimamia haki msingi na usalama wa wahamiaji. Takwimu zinaonesha kwamba, Mashirika ya kidini ni kati ya taasisi ambazo zimekuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.