2014-04-14 09:29:22

Wakazi wa Roma mwaalikwa kushiriki Ibada ya Njia ya Msalaba- Koloseo Roma


Wakazi wa Jiji la Rome, nyote mnaalikwa siku ya Ijumaa Aprili 18, majira ya jioni kujiunga katika Ibada ya Njia ya Msalaba, katika magofu ya Koloseo, itakayoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko. Katika Ibada hiyo tafakari zinaulenga mgogoro wa kiuchumi na hali ya wahamiaji wanaopambana na maovu mbalimbali kimaisha hasa kwa vijana wengi.

Vijitabu vya Tafakari vinachapishwa Jumanne hii na Taasisi ya uchapishaji ya Libreria Editrice Vaticana, kama ilivyoandikwa na Msgr. Giancarlo Bregantini , Askofu Mkuu wa Campobasso - Boiano , Kusini mwa Italia ambako kumekuwa na matukio mengi ya kusikitisha ya wahamiaji wanaotafuta kuingia Italia. Katika tafakari hiyo anasema, vituo 14 vya Mateso ya Yesu , pia ni sawa na mapigo ya dunia ya leo hasa matukio ya wahamiaji na mateso ya watu, kama inavyojulikana kwa wachungaji wa Jimbo la Kusini mwa Italia, ambako kumetokea mauaji yaliyosababishwa na sumu zinazo toka katika taka, hali ya wafungwa wanaoishi katika msongamano mkubwa magerezani, na wahamiaji.

Askofu Mkuu Giancarlo Bergantini anasema , ndani ya mti wa msalaba wa Kristo, mna dhambi zote za watu , ikiwemo ukiukwaji wa haki zinazozalishwa na mgogoro wa kiuchumi, na matokeo yake makubwa ya kijamii , kama vile uhaba wa kazi , ukosefu wa ajira ,ughushi wa fedha , watu kujiua , rushwa na ufisadi. Yesu aliyabeba yote hayo wakati akitembea katika njia ya mateso ya Kalvario, kwa ajili ya kutufundisha kwamba, ndani ya maisha si kutoa jibu ovu kwa uovu lakini ni kujenga madaraja ya mshikamano, na kuishinda hofu ya kutengwa , na kutafuta nguvu mpya za kisiasa kwa ajili ya utafutaji majibu kwa matatizo ya kijamii kwa njia amani na maridhiano.


Askofu Mkuu Bergantini anaendelea kuitafakari njia ya Msalaba katika eneo la Koloseo, hasa akilenga katika mapigo ya dunia ya leo, na hasa hali ya wakimbizi na wahamiaji, majeraha ya wanawake ambao ni waathirika wa unyanyasaji, viwewe vya watoto waliodhulumika kijinsia, maumivu ya mama wale ambao wamepoteza watoto wao katika vita, katika dimbwi la madawa ya kulevya au ulevi wa pombe kupindukia.
Lakini anasema, kuanguka kwa Yesu mara tatu katika njia ya Golgotha ​​, kunatupatia mawazo ya uhakika yenye matumaini katika kuyashinda majaribu. Hii ni sala kali kwa Mungu, aliyoitoa Yesu, kwa ajili ya kuwaangazia wale wanaoutazama msalaba wake. Na hivyo sisi tunajifuza kutoka kwa Kristo kukubali udhaifu, na kukataa kukatishwa tamaa au kushindwa na ovu lolote. Badala yake, tuwe kama Simoni wa Krene , mtu ambaye alimsaidia Mwana wa Mungu kuubeba msalaba, ambaye leo hii pia anatuambia kwamba, ni kukutana na kila mmoja na kutoa msaada kujenga udugu, na kumgundua Mungu katika kila mwanadamu.









All the contents on this site are copyrighted ©.