2014-04-14 09:38:04

Ugonjwa wa kifua kikuu bado ni tishio kwa maisha ya watu wengi!


Shirika la Afya Duniani, WHO linasema, ugonjwa wa kifua kikuu bado ni hatari sana duniani na unaendelea kuongezeka kwa kasi kubwa kwani kila mwaka kuna wagonjwa wapya wa Kifua kikuu millioni tisa. Kifua kikuu ni ugonjwa ambao umeendelea kuwa sugu kwa dawa nyingi. Inakadiriwa kwamba, kuna watoto millioni moja duniani ambao wameambukizwa ugonjwa wa Kifua kikuu. RealAudioMP3

Jambo la kusikitisha wanasema wataalam wa ugonjwa wa Kifua kikuu ni kwamba, watu wanaendelea kupuuzia uwepo wa ugonjwa huu licha ya madhara yake makubwa katika afya za watu. Zaidi ya wagonjwa 450, 000 wana sumbuliwa na ugonjwa wa Kifua kikuu sugu, wadudu ambao wanaweza kutibiwa kwa uhakika kwa asilimia 20% tu.

Utafiti wa ugonjwa wa Kifua Kikuu uliofanywa kwenye Chuo Kikuu cha Havard, Marekani na kuchapishwa kwenye Jarida la “Lancet” unaonesha kwamba, Bara la Asia lina idadi kubwa ya watoto wanaosumbuliwa na ugonjwa wa kifua kikuu, Idadi yao inakadiriwa kufikia watoto 400, 000.

Bara la Afrika lina watoto wenye ugonjwa wa Kifua kikuu zaidi ya 280, 000. Ugonjwa wa Kifua kikuu Barani Ulaya unaendelea kupungua sana na kwamba, kwa sasa kuna mpango mkakati wa kufuta kabisa ugonjwa wa Kifua kikuu Barani Ulaya, ifikapo mwaka 2050. Wataalam wa ugonjwa wa Kifua kikuu wanasema, mapambano bado yanaendelea na kwa sasa wameandaa “Skadi Mpya 10” zitakazorushwa hivi karibuni kama sehemu ya mchakato wa kupambana na ugonjwa wa Kifua kikuu ambao bado unaendelea kuwa ni tishio.

Makampuni 50 yanaendelea kufanya utafiti kuhusu uhakika wa Skadi hizi katika kutibu na kuponya ugonjwa wa Kifua kikuu. Ili kufanikisha tafiti mbali mbali kuhusu ugonjwa wa Kifua kikuu bado kuna upungufu wa dolla millioni 1.5 kila mwaka.








All the contents on this site are copyrighted ©.