2014-04-14 14:38:11

Juma kuu ni wakati muafaka wa kuungama dhambi!


Mama Kanisa amelianza Juma kuu kwa maandamano makubwa Jumapili ya Matawi pamoja na kukumbuka Mateso ya Kristo Msalabani kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti. Alhamisi kuu, Mama Kanisa anakumbuka siku ile iliyotangulia kuteswa kwake, Yesu alipoweka Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Daraja Takatifu, Sakramenti zinazomwilishwa katika huduma ya mapendo na udugu. Hii ni siku ambayo Makleri wanarudia tena ahadi zao za utii kwa Maaskofu mahalia pamoja na kubariki mafuta matakatifu.

Ijumaa kuu, Mama Kanisa anakumbuka kwa namna ya pekee kabisa, mateso na kifo cha Kristo Msalabani. Hapa Msalaba unaonesha: hekima, huruma na upendo wa Mungu kwa mwanadamu. Jumamosi kuu, Mama Kanisa anakaa katika kimya kikuu, ili kusubiria Ufufuko wa Kristo kutoka katika wafu, tayari kumwimbia Alelluiya kuu kwa kumshangilia, mwaliko kwa waamini kufa na kufufuka na Kristo kwa kuikata dhambi na nafasi zake.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii anasema kwamba, Juma kuu ni muda uliokubalika kwa waamini kumuungamia Mungu dhambi zao na kuanza kutembea katika njia nyofu!







All the contents on this site are copyrighted ©.