2014-04-11 08:37:05

Siku za Vijana Duniani zinapania kukuza na kudumisha ari na moyo wa kimissionari


Baba Mtakatifu Francisko ana matumaini makubwa katika maadhimisho ya Siku za Vijana Duniani kama nyenzo msingi inayopania kuwasha na kukuza ari na moyo wa kimissionari miongoni mwa vijana ndani ya Kanisa. Ni maneno ya Kardinali Stanislaw Rylko, Rais wa Baraza la Kipapa la Walei, wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kimataifa wa wakurugenzi wa utume wa vijana, unaofanyika mjini Roma kuanzia tarehe 10 hadi tarehe 13 Aprili 2014. Mikutano hii ni sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani itakayoadhimishwa Jimbo kuu la Krakovia, Poland, kunako mwaka 2016.

Mkutano huu unahudhuriwa na wajumbe 250 kutoka katika Mabaraza ya Maaskofu Katoliki 90 na Jumuiya za Kitume 45 sanjari na Kamati ya Maandalizi ya Siku ya Vijana Duniani Rio de Janeiro na Kamati kutoka Jimbo kuu la Krakovia. Kardinali Rylko anasema, katika maadhimisho ya Siku ya Vijana Kijimbo, itakayofanyika Jumapili ya Matawi, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Baba Mtakatifu Francisko atawakabidhi rasmi vijana kutoka Poland Msalaba wa Siku ya Vijana Duniani, uliotembezwa nchini Brazil kama sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani yaliyokofanyika nchini Brazil.

Tukio hili ni muhimu sana kwa mwaka huu, kwani Mama Kanisa anaadhimisha kumbu kumbu ya Miaka thelathini, tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, kunako Mwaka 1984 wakati wa Siku kuu ya Pasaka sanjari na kufunga rasmi Mwaka wa Ukombozi, alipowakabishi vijana Msalaba wa Mwaka wa Ukombozi. Ni Msalaba ambao umetembezwa sehemu mbali mbali za dunia kwa kuwasindikiza vijana katika shida na mahangaiko yao bila kusahau furaha na matumaini yao kwa Kristo na Kanisa lake.

Msalaba wa Mwaka wa Ukombozi, umekuwa ni alama ya toba na wongofu wa ndani, chemchemi ya miito mitakatifu ndani ya Kanisa na kwamba ni Msalaba ambao kweli umekuwa ni kikolezo cha imani na matumaini miongoni mwa vijana wa kizazi kipya. Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani, kama alivyosema Baba Mtakatifu Francisko nchini Brazil ni maadhimisho ya imani na udugu na kwamba, hii ni zawadi kubwa kwa Mama Kanisa.

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016 yatafanyika nchini Poland, miaka 25 tangu yalipofanyika kwa mara ya kwanza nchini Poland kunako mwaka 1991 mara tu baada ya kuanguka kwa Ukuta wa Berlin. Hapo dunia ikashuhudia nguvu na jeuri ya vijana waliomiminika kutoka sehemu mbali mbali za dunia ili kuungana katika maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani, kwa pamoja wakaimba, ule wimbo maarufu "AbbĂ , Padre", unaoendelea kuvuma sehemu mbali mbali za dunia.

Tangu wakati huo anasema Kardinali Rylko, kumekuwepo na mabadiliko makubwa sana ulimwenguni na ndani ya Kanisa. Kuna mabadiliko makubwa katika ulimwengu wa vijana wanaoogelea katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Kumbe, maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani ni kikolezo cha ari na mwamko wa kimissionari, kwa kutafuta na kuibua mbinu mkakati kwa ajili ya utume wa Mama Kanisa kwa vijana.

Kwa namna ya pekee, wakati huu, Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kukazia umuhimu wa upendo na huruma ya Mungu; toba na wongofu wa ndani. Mama Kanisa anajiandaa kuadhimisha tukio la kihistoria kwa kuwatangaza Wenyeheri Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuwa watakatifu hapo tarehe 27 Aprili 2014. Kanisa katika maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani itakayofanyika nchini Poland kunako mwaka 2016, itamkumbuka Papa Yohane Paulo II muasisi wa Siku za Vijana na Msimamizi wa maadhimisho ya Siku za Vijana Duniani.

Mwenyeheri Yohane Paulo II kwa vijana ataendelea kuwa ni Baba na Rafiki; Mlezi na Msimamizi wa vijana mbinguni. Mkutano huu umefanya pia tathmini ya maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani iliyofanyika Rio de Janeiro, Brazi, pamoja na kuangalia matunda ya shughuli za kichungaji yaliyopatikana wakati wa maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani nchini Brazil kwa njia ya ushuhuda na taarifa mbali mbali zilizowasilishwa na wajumbe.







All the contents on this site are copyrighted ©.