Lindeni na kutetea zawadi ya uhai kwa ujasiri na upendo mkuu
Baba Mtakatifu Francisko anawashukuru wajumbe wa Chama cha Maisha nchini Italia kwa
kuonesha ukarimu na mshikamano wa pekee ambao umesaidia katika kipindi cha miaka ishirini
kuokoa maisha ya watoto ambao pengine wasingebahatika kuona mwanga wa jua. Ni Chama
ambacho kimekuwa mstari wa mbele kulinda na kutetea uhai tangu pale mtoto anapotungwa
mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mapenzi ya
Mungu.
Baba Mtakatifu Francisko ameyasema hayo, Ijumaa, tarehe 11 Aprili 2014
alipokutana na kuzungumza na wanachama wa Chama cha Maisha nchini Italia. Anasema,
maisha ya mwanadamu ni matakatifu na yanapaswa kuheshimiwa na kulindwa ni haki msingi
ya kibinadamu, ambayo inafumbata haki nyingine zote na wala haifungwi na hali, ubora,
au siasa.
Amri ya Mungu inayosema usiue inatetea zawadi ya uhai, changamoto
kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kukataa kukumbatia uchumi unaowatenga
na kuwaua watu; uchumi unaompima mwanadamu kwa mizani ya bidhaa, hali inayoonesha
utamaduni usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya wengine, kiasi cha kuendeleza mchezo
huu mchafu katika uhai wa mwanadamu.
Baba Mtakatifu anasema hatari kubwa inayomkumbwa
mwanadamu katika ulimwengu mamboleo ni tatizo la kutenganisha uchumi na kanuni maadili;
uwepo wa soko huria linaoongozwa na nguvu ya soko pamoja na mabadiliko ya kiteknolojia.
Kanuni maadili si jambo linalopewa msukumo wa pekee kama dira na mwongozo wa shughuli
za kiuchumi. Hii ni changamoto kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusimama
kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai, tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni
mwa mama yake, hadi mauti ya kawaida yanapomfika.
Mababa wa Mtaguso mkuu wa
Pili wa Vatican wanakumbusha kwamba, uhai ukishatungwa, lazima uhifadhiwe kwa juhudi
kubwa; kwa hiyo kuharibu mimba na kuwauwa watoto ni mauaji ya kuchukiza kabisa. Wakristo
wanachangamotishwa kuwa ni mashahidi wa wa Kiinjili kwa kutetea na kulinda zawadi
ya uhai kwa ujasiri na upendo mkuu katika hatua zake zote.
Baba Mtakatifu
anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa karibu na wanawake wenye shida
na mahangaiko yao ya ndani; kwa kuwaheshimu, kuwasikiliza, kuwapokea na kuwasindikiza
katika utume wao.