2014-04-10 07:56:32

Jumuiya ya Kimataifa na kamatakamata ya Wasomali nchini Kenya


Jumuiya ya Kimataifa imesikitishwa sana na operesheni kamatakamata iliyofanywa na Serikali ya Kenya dhidi ya Wakimbizi kutoka Somalia kama sehemu ya mkakati wa kulinda na kudumisha amani na utulivu dhidi ya mashambulizi yanayofanywa na vikundi vya kigaidi nchini Kenya.

Serikali ya Kenya kwa upande wake imeeleza kwamba, operesheni hii inalenga kuvunja nguvu za vikundi vya kigaidi ambavyo vimeendelea kutishia amani na usalama wa wananchi wa Kenya kwa siku za hivi karibuni, kiasi kwamba, wananchi hawana tena na uhakika wa usalama wa maisha na mali zao. Walengwa wakuu ni Kikundi cha kigaidi cha Al Shabaab, ambacho kimepelekea watu kadhaa wakiwemo wanawake na watoto kukamatwa na kuwekwa kwenye uwanja wa mpira. Taarifa hizi zimethibitishwa na Kamanda mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Kenya Bwana Benson Kibue.

Shirika la kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa linasema, limejitahidi kushauri utoaji wa huduma kwa wakimbizi na wafungwa wa kisiasa wanaotaka kupata hifadhi ya kisiasa, nchini Kenya lakini bila mafanikio. Jumuiya ya Kimataifa inaitaka Serikali ya Kenya kuzingatia na kuheshimu sheria za kimataifa na kwamba, watu waliokamatwa wanapaswa kutendea kama binadamu na wala si kubaguliwa.







All the contents on this site are copyrighted ©.