2014-04-10 14:48:39

Biashara haramu ya binadamu ni janga na uhalifu dhidi ya ubinadamu!


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi, tarehe 10 Aprili 2014 amekutana na kuzungumza na washiriki wa mkutano wa pili wa mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu ulioandaliwa mjini Vatican na Taasisi ya Kipapa ya Sayansi. Baba Mtakatifu anasema, biashara haramu ya binadamu ni janga katika maisha ya mwanadamu wa leo, ni uhalifu dhidi ya binadamu.

Baba Mtakatifu anasema kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kuunganisha nguvu zake, ili kuibua mbinu mkakati, weledi na ujuzi kwa kuguswa na huruma ya kiinjili ili kuwasaidia wahanga na hatimaye, kukomesha biashara haramu ya binadamu. Vikosi vya ulinzi na usalama vinapaswa kutekeleza wajibu wake kwa kuzingatia sheria pamoja na kushirikiana na wadau mbali mbali, wanaotoa huduma ya kuwapokea na kuwahifadhi waathirika.

Baba Mtakatifu anawaalika wadau kujadiliana, kushirikishana na hatimaye, kukamilishana katika mchakato wa mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu, kumbe mikutano kama hii ni ya maana na ni muhimu sana. Baba Mtakatifu anawashukuru wadau kwa kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja, anawatakia kheri na mafanikio mema katika shughuli zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.