Papa Francisko kuadhimisha Ibada ya Alhamisi kuu jioni na walemavu
Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu, Alhamisi
kuu jioni, tarehe 17 Aprili 2014, kwenye Jumuiya ya Mfuko wa Don Gnochi, iliyoko mjini
Roma. Siku ya Alhamisi kuu jioni, Mama Kanisa anaadhimisha Ibada ya Misa Takatifu
kama sehemu ya kumbu kumbu endelevu ya Siku ile Yesu alipoweka Sakramenti ya Ekaristi
Takatifu sanjari na Sakramenti ya Daraja Takatifu, zinazomwilishwa katika huduma ya
upendo hasa kwa watu wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Jumuiya hii inawahudumia
watu wenye matatizo ya afya wanaohitaji msaada wa pekee ili kuweza kurudia tena katika
hali yao ya kawaida na kuingizwa tena katika maisha ya kijamii. Kimsingi ni watu wenye
ulemavu, ambao wanapewa huduma kwenye Jumuiya hii ya Don Gnochi. Katika Ibada hiyo
itakayoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko, wagonjwa, jamaa, wafanyakazi na uongozi
wa kituoni hapo watashiriki.