2014-04-09 08:25:46

Papa anahitaji kupata ushauri kutoka kwa Maaskofu wenzake


Papa Paulo VI kunako tarehe 15 Septemba 1965, baada ya kusoma alama za nyakati na kutambua mahitaji ya Kanisa, akaamua kwa ujasiri mkubwa kuimarisha umoja na mshikamano kati ya Khalifa wa Mtakatifu Petro na Maaskofu mahalia, waliopewa dhamana ya kuliongoza Kanisa, akaamua kwa utashi wake mwenyewe kuanzisha Sinodi za Maaskofu, kama chombo makini cha ushauri kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Sinodi kimsingi ni matunda ya Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Tangu wakati huo, Mama Kanisa ameendelea kuadhimisha Sinodi za Maaskofu ambazo zimetoa mchango mkubwa katika maisha na utume wa Makanisa mahalia na Kanisa na Kiulimwengu kwa kuangalia fursa, matatizo na changamoto zinazolikabili Kanisa, ili kutafutiwa ufumbuzi wa pamoja. Sinodi za Maaskofu zimekuwa ni msaada mkubwa na pia zimetoa ushauri wa kulinda na kuimarisha imani kwa ari, moyo mkuu na ujasiri katika maisha ya Kikristo sanjari na kuimarisha nidhamu ya maisha ndani ya Kanisa.

Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili kwa kutambua umuhimu na dhamana ya Sinodi za Maaskofu, alikwishaona kwamba, kulikuwa na haja ya kufanya maboresho makubwa katika Maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu, kwa kuongeza mshikamano wa kichungaji katika Sinodi za Maaskofu. Kumbe, Sinodi za Maaskofu ni mwendelezo wa Fumbo la Kanisa la Mungu linalojikita katika umoja na utume. Haya ni kati ya mambo yanayopaswa kupewa msukumo wa pekee kabisa kwa nyakati hizi.

Hivi ndivyo anavyoandika Baba Mtakatifu Francisko katika barua yake kwa Kardinali Lorenzo Baldisseri, Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu, baada ya kufanya uamuzi wa kumpandisha hadhi Monsinyo Fabio Fabene, Katibu mkuu msaidizi kuwa Askofu. Papa anasema, imekwisha yoyoma takribani miaka hamsini tangu Sinodi za Maaskofu zilipoanzishwa kwa kusoma alama za nyakati wakati huu anapotekeleza dhamana na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, anapenda kuonesha mshikamano wake wa dhati na Maaskofu wote wa Makanisa mahalia kama njia ya kuenzi urithi wa Sinodi kutoka kwa Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko anasema katika ukweli na uwazi kwamba, Khalifa wa Mtakatifu Petro anahitaji uwepo endelevu wa Maaskofu wenzake, ili kupata ushauri, hekima na mang'amuzi, ili wote kwa pamoja waweze kukiri kwamba, kwa hakika Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu aliye hai, sanjari na kuwa makini kusikiliza sauti ya Roho Mtakatifu kwa ajili ya Kanisa lake. Anawashukuru wote walioachangia na wale wanaoendelea kuchangia katika kuendeleza na kudumisha Maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu.







All the contents on this site are copyrighted ©.