2014-04-09 09:36:08

Mshikamano na umoja kati ya Maaskofu Katoliki


Kardinali Lorenzo Baldisseri Katibu mkuu wa Sinodi za Maaskofu anasema, Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa Kitume Injili ya Furaha, Evangelii Gaudium, EG., ambao unachota utajiri wake kutoka katika Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya iliyofanyika mjini Vatican Oktoba 2012, anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuonja Furaha ya Injili inayotangazwa na Mama Kanisa katika utekelezaji wa dhamana yake ya Kimissionari sehemu mbali mbali za dunia. RealAudioMP3
Baba Mtakatifu ametafakari kwa kina na mapana Mapendekezo yaliyotolewa na Mababa wa Sinodi juu ya Uinjilishaji Mpya, akayachambua na hatimaye akayaingiza kwenye Waraka wake wa Kitume, Injili ya Furaha. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kuwatangazia jirani zao Injili Furaha. Waraka huu ni matunda pia ya tafakari ya Neno la Mungu, Mafundisho ya Mababa wa Kanisa na Nyaraka mbali mbali zilizokwishatolewa na watangalizi wake pamoja na baadhi ya waandishi na wataalimungu wanaogusa changamoto za Uinjilishaji katika ulimwengu mamboleo.
Kardinali Baldisseri anaendelea kubainisha kwamba, Waraka huu unafanya rejea ya kina mintarafu nyaraka za Mabaraza ya Maaskofu Mahalia na Sinodi za Mapatriaki. Hapa Baba Mtakatifu anapenda kukazia umuhimu wa Sinodi kama chombo muhimu sana kinachoweza kumsaidia Khalifa wa Mtakatifu Petro kutekeleza wajibu wake katika maisha na utume wa Kanisa la kiulimwengu, bila kusahau mchango wa kina unaotolewa na Mabaraza ya Maaskofu mahalia. Baba Mtakatifu anaitaka Familia ya Mungu kufanya wongofu wa kichungaji, unaojikita katika asili ya Kanisa linalotumwa kwenda kutangaza Injili ya Furaha. Wongofu wa kichungaji unamgusa hata Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Hili ni wazo endelevu kutoka kwa Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ambalo kwa sasa halina budi kufanyiwa kazi kama kielelezo makini cha umoja na mshikamano wa Kanisa, kama walivyosema Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican “Collegiality”. Ni suala linalogusa Mafundisho Tanzu ya Kanisa na Madaraka ndani ya Kanisa. Ni dhana inayokazia umuhimu wa majadiliano ya Kiekumene na kwamba, Wakatoliki wanayo nafasi ya kujifunza zaidi umuhimu wa umoja na mshikamano wa kiaskofu na mang’amuzi ya umuhimu wa Sinodi kutoka kwa Makanisa ya Mashariki.
Baba Mtakatifu Francisko yuko makini na anafahamu kile kinachoendelea katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia hususan katika sekta ya elimu, afya na njia za mawasiliano ya jamii. Katika miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na maendeleo makubwa ya teknolojia ya mawasiliano, kiasi kwamba, ulimwengu kwa sasa unafanana kama Kijiji. Baba Mtakatifu anatambua fika athari za ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Watu wanapata mafuriko ya habari na takwimu na kwamba, wote wanatendewa haki sawa, hali ambayo wakati mwingine inasababisha kinzani na mmong’onyoko wa tunu msingi za kimaadili.
Kutokana na changamoto hizi, anasema Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii kwamba, kuna haja ya kuwa na majiundo makini katika sekta ya elimu yatakayowawezesha watu kuwa na upeo mpana zaidi katika matumizi ya maendeleo haya kwa kuzingatia tunu msingi za maisha adili na utu wema.
Baba Mtakatifu anawachangamotisha waamini kutoka huko walikojificha na kuanza hija ya mchakato wa kukutana na watu wengine ili kuwashirikisha Injili ya Furaha kwa kuishi, kushikamana na kutaabikiana pamoja. Kweli za Kiinjili hazina budi kuwasilishwa kikamilifu kwa kutambua kwamba, wakati mwingine Kweli za Kiinjili hazipewi umuhimu na uzito unaostahili.
Watangazaji wa Injili wanapaswa kufikisha ujumbe kwa hadhira inayokusudiwa kwa ufasaha, ili Injili iweze kugusa sakafu ya mioyo ya watu. Hapa Baba Mtakatifu anawataka Wainjilishaji kujikita katika mambo msingi, yaliyo mazuri na muhimu; yenye mvuto na mashiko na kwamba, yanafumbata ukweli. Kweli za Kiinjili ziwafikie watu wa kawaida ili waguswe na kuvutika na Injili ya Furaha, kwani Neno la Mungu lina nguvu na linatoa hamasa.








All the contents on this site are copyrighted ©.