2014-04-09 14:33:08

Karama za Roho Mtakatifu


Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Katekesi yake, Jumatano tarehe 9 Aprili 2014, kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican uliokuwa umefurika kwa umati mkubwa wa watu, ameanza Katekesi mpya inayofanya tafakari kuhusu karama za Roho Mtakatifu. Ikumbukwe kwamba, Roho Mtakatifu mwenyewe ni zawadi ya Mungu, inaonesha kwa namna ya pekee upendo wa Mungu ndani ya Kanisa na katika mioyo ya waamini.

Kwa kuzingatia unabii uliotolewa na Nabii Isaya, Mama Kanisa katika Mapokeo yake anatambua karama saba za Roho Mtakatifu: Hekima na Akili; Ushauri na Nguvu; Ufahamu, Maarifa na Uchaji wa Mungu. Baba Mtakatifu anasema, Hekima ndiyo Karama ya kwanza katika orodha hii. Hii ni karama ya maisha ya kiroho, ni mwanga wa maisha ya mtu na nuru inayomwezesha mwamini kutafakari mambo ya kimungu kwa jicho la kimungu kwa moyo wa unyenyekevu kadiri ya maongozi ya Roho Mtakatifu.

Hekima ni karama inayoibuliwa kwa kuwa karibu zaidi na Mwenyezi Mungu kwa njia ya sala na mshikamano wa upendo. Ni karama inayomwezesha mwamini kutambua kwa furaha mpango wa Mungu katika mambo yote. Hekima ya maisha ya Kikristo ni neema ya Mungu na uwezo wa kutambua uwepo na uzuri wake unaowazunguka watu wake.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, dunia ya leo ina kiu ya kuona watu wakitolea ushuhuda wa karama hii. Huu ni mwaliko wa kusali ili kumwomba Mwenyezi Mungu aweze kuwakirimia waja wake karama hii, ili kwa kufurahia katika Roho Mtakatifu, waamini wanaweza kuwa kweli ni watu wa Mungu; wakiwa wazi kwa hekima na nguvu ya upendo wake unaokoa.

Baba Mtakatifu anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanayapatia maisha yao ladha ya uwepo wa Mungu, kwa njia ya Roho Mtakatifu waweze kung'amua mema na mabaya; kwa kumtambua Mungu katika yote kwa kuwaonjesha wengine upendo na huruma yake. Anawataka waamini kukua na kukomaa katika hekima ya Kimungu, ili waweze kuwa kweli ni wataalam wa mambo ya Kimungu kwa kuwashirikisha jirani zao.

Baba Mtakatifu anasema, Roho Mtakatifu anawafundisha waamini na kuwapatia hekima na Ukweli wa Kristo. Huu ni mwaliko wa kumkimbilia mara kwa mara ili waamini hao waweze kuwa ni Wafuasi kweli wa Yesu Kristo. Kipindi hiki cha Kwaresima ni fursa ya kumwomba Mungu msamaha kwa kushiriki kikamilifu katika Sakramenti ya Upatanisho. Wagonjwa waunganishe mateso na mahangaiko yao katika Msalaba wa Kristo; wanandoa wasameheane na kusaidiana wao kwa wao.







All the contents on this site are copyrighted ©.