2014-04-08 09:12:31

Washeni nyoyo za watu kwa upendo na ukarimu kutoka kwa Yesu na Kanisa lake!


Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru wajumbe wa kamati ya Maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani iliyofanyika mjini Rio de Janeiro, Brazil kwa kusema kwamba, ni hija ya kichungaji ambayo itakuwa vigumu sana kwake kuisahau. Hii ni kutokana na mapokezi makubwa, ukarimu na majitoleo ya wanachi wa Brazil waliomwonjesha na kumshirikisha, kiasi kwamba, upendo wa Mungu ukaweza kupenya katika mioyo ya mamillioni ya vijana waliokuwa wamekusanyika mjini Rio de Janeiro.

Baba Mtakatifu anasema, alipofika nchini Brazil aliwaomba wananchi wa Brazil kumpokea na kumkaribisha miongoni mwao na kwamba, aliporejea tena mjini Roma, alibaki na hamu ya kutaka kubaki Brazil. Anawashukuru wote walioachangia kwa hali na mali katika kufanikisha Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani. Kuna watu wamejisadaka, wamekumbana na kinzani, lakini yote yamekwenda vyema kadiri ya mpango wa Mungu, licha ya mapungufu na ukosefu wa rasilimali.

Hivi ndivyo Yesu alivyofanya alipowalisha watu elfu tano kwa mikate mitano na samaki wawili, changamoto ya kusonga mbele kwa imani na matumaini kwa kuendelea kumtegemea Mwenyezi Mungu. Upendo wa Kristo unawawajibisha waamini kuendelea kuonesha mshikamano na watu wanaoishi katika mazingira magumu ili waweze kuonja urafiki unaobubujika kutoka kwa Yesu. Baba Mtakatifu anawataka wanakamati hawa kusonga mbele pasi na woga ili kuwahudumia watu.

Kanisa linapaswa kujikita katika ari na moyo wa kimissionari ili kuwatangazia watu Injili ya Furaha pasi na woga wala kujibakiza kwa ajili ya Injili ya Kristo. Ili kutekeleza wajibu huu, Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumwangalia Mtakatifu Yosefu wa Anchieta, mtume wa Brazil aliyetangazwa hivi karibuni kuwa Mtakatifu anayesema kwamba, si vigumu kwa wale wanaowafaraji wengine wakiwa na lengo la kuonesha utukufu wa Mungu na wokovu wa roho za watu, kiasi hata cha kuthubutu kutoa maisha yao.

Baba Mtakatifu anawaalika wajumbe wa Kamati ya Maandalizi ya Siku ya Vijana Duniani nchini Brazil kusonga mbele kwa furaha na ujasiri wa kuwasha nyoyo za wananchi wa Brazil kwa upendo wa Yesu na Kanisa lake.







All the contents on this site are copyrighted ©.