Kardinali Leonardo Sandri pamoja na wafanyakazi wote wa Baraza la Kipapa la Makanisa
ya Mashariki anapenda kutuma salam zake za rambi rambi kutokana na mauaji ya Padre
Frans Van Der Lugt, SJ, aliyekuwa na umri wa miaka 75 yaliyotokea huko Homs, Syria,
tarehe 6 Aprili 2014. Anasema mauti yamemfika Padre Frans wakati Jumuiya ya Waamini
wa Makanisa ya Mashariki walikuwa wamekusanyika kwa ajili ya kuombea amani huko Mashariki.
Haya ni mauaji yanayoendelea kufanywa dhidi ya watu wasiokuwa na hatia nchini Syria.
Padre Frans Van Der Lugt amekuwa nchini Syrua tangu mwaka 1966 na hivi karibuni
alizungumza katika ukweli na uwazi juu ya mateso na mahangaiko ya wananchi wanaoishi
huko Homs. Baraza la Kipapa la Makanisa ya Mashariki linaiomba Jumuiya ya Kimataifa
kusaidia mchakato wa kurudisha amani na utulivu huko Syria, kwani watu wengi wanaendelea
kupoteza maisha na wengi wengi wanalazimika kuyakimbia makazi yao.