2014-04-07 14:35:41

Ujumbe wa Papa Francisko kwa Maaskofu Katoliki Tanzania


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 7 Aprili 2014 amekutana na kuzungumza na Maaskofu Katoliki Tanzania ambao wako kwenye hija ya kitume mjini Vatican kama kielelezo cha kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Anasema, Kanisa la Tanzania limebahatika kuwa na historia inayojikita katika dhana ya Umissionari, inayowasukuma watoto wa Kanisa kujitosa kimasomaso kuwatangazia wengine Injili ya Furaha.

Hii ni changamoto ya kuhakikisha kwamba, Kanisa la Tanzania linakuza ari na mwamko wa Kimissionari, ili kweli za Kiinjili ziweze kupenya katika medani mbali mbali za maisha, ili kuandika ukurasa mpya wa historia ya Uinjilishaji nchini Tanzania. Uinjilishaji bado unaendelea kujionesha nchini Tanzania katika maisha na utume wa Kanisa; katika maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa, maisha ya kisakramenti, mchango wa Kanisa katika sekta ya elimu na afya, Katekesi na maisha ya kawaida ya Wakristo.

Huu ni mwaliko kwa waamini kutolea ushuhuda wa maisha yao kwa kumtangaza Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Hii ndiyo changamoto kubwa anasema Baba Mtakatifu kwa wakristo nchini Tanzania, kuhakikisha kwamba, wanakuwa ni mashuhuda wa upendo wa Kristo unaomkomboa mwanadamu, kwa kumwilishwa na kuadhimishwa na waamini ndani ya Kanisa.

Baba Mtakatifu Francisko analishukuru Kanisa Katoliki Tanzania kwa kuendelea kutolea ushuhuda wa kimissionari kwa kuwahudumia wagonjwa wa Ukimwi pamoja na kuwajengea uwezo wa kupambana na Ukimwi kwa kuwajibika barabara na kudumisha maadili mema. Analishukuru Kanisa kwa kujikita katika maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Baba Mtakatifu anawaombea Wakristo nguvu, hekima na utakatifu wa Wamissionari wa kwanza uendelee kulihamaisha Kanisa kuwa kweli ni kielelezo cha ushuhuda wa Kristo na Kanisa lake.

Baba Mtakatifu anasema, ili Kanisa liweze kweli kutekeleza utume wake wa: kufundisha, kutakatifuza na kuongoza, linawahaitaji Mapadre wasomi, wema na watakatifu; ni watu wanaohitaji kupatiwa majiundo makini ya awali na endelevu: kiutu, kiroho, kiakili na kichungaji, ili waweze kuendelea kuwa kweli ni watumishi waaminifu kwa ahadi walizoweka wakati walipopokea Sakramenti ya Daraja Takatifu. Majiundo endelevu yajikite katika wongofu na upendo katika shughuli za kichungaji na kwa njia hii wanaweza kuwa kweli ni vyombo vya mageuzi ya maisha ya kiroho katika Parokia kwa kuonesha umoja na mshikamano; kivutio kikuu kwa vijana wanaotaka kujitosa ili kumtumikia Kristo na Kanisa lake kwa njia ya Daraja Takatifu la Upadre.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuhimiza dhamana na ushiriki wa waamini walei katika maisha na utume wa Kanisa kama ilivyojionesha na kusisitiziwa kwenye Kongamano la Ekaristi Takatifu Kitaifa lililofanyika kunako Mwaka 2012 pamoja na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Haya ni matukio muhimu katika kukuza na kuimarisha imani ya Watu wa Mungu nchini Tanzania. Makatekista wanapaswa kupongezwa zaidi kwa kuwatangazia jirani zao Injili pamoja na kuwashirikisha utimilifu wa maisha na mafundisho ya Kikristo.

Baba Mtakatifu anasema, hizi ni nyenzo msingi katika kupambana na imani za kishirikina, madhehebu yenye misimamo mikali pamoja na mawazo mepesi mepesi, lakini jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, waamini wanashirikisha vijana uzuri na utajiri wa imani ya Kanisa Katoliki. Kila mwamini awe ni chachu ya kuleta mabadiliko ndani ya Jamii na kwamba, waamini walei waliofundwa barabara wanaweza kuwa ni vielelezo vya utu na maadili mema katika tamaduni na kazi za watu, changamoto endelevu kwa nyakati hizi.

Baba Mtakatifu Francisko katika hotuba yake kwa Maaskofu Katoliki Tanzania amekazia pia umuhimu wa kuendelea kuinjilisha Familia, kwa kutambua kwamba, hiki ni kiini cha Uinjilishaji Mpya kama wanavyokazia Mababa wa Sinodi Maalum ya Maaskofu iliyofanyika kunako Mwaka 2009. Familia zijengewe moyo na ari ya kusali, uaminifu katika maisha ya ndoa ya mke mmoja, usafi wa roho na unyenyekevu katika huduma, kwa kutambua kwamba, Kanisa Katoliki nchini Tanzania linaendelea kuchangia katika ustawi na mafao ya wengi katika sekta ya elimu na afya, mambo msingi katika ujenzi wa utulivu na maendeleo ya nchi.

Kanisa lisimame kidete kushuhudia utakatifu wa maisha ambayo ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, dhamana inayoweza kuendelezwa na familia thabiti kama sehemu ya mchakato wa kuwaandaa vijana wa kizazi kipya ili kukabiliana na changamoto za maisha kwa: hekima, ujasiri na ukarimu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, anaridhishwa na jitihada zinazofanywa nchini Tanzania kuhakikisha kwamba kuna kuwepo na uhuru wa kuabudu; kwa kuheshimu na kuzingatia haki msingi za binadamu; uhuru wa dhamiri nyofu sanjari na kuheshimu utu wa mwandamu. Yote haya yanapania umoja wa kitaifa, amani na mafao ya wengi.

Baba Mtakatifu analipongeza Kanisa Katoliki Tanzania kwa kuendeleza mchakato wa msamaha, amani na majadiliano kati ya watanzania ambao kwa wakati mwingine wanakabiliana na madhulumu na matumizi ya nguvu. Umoja na mshikamano katika maisha na sala ni nguvu thabiti katika kukabiliana na changamoto hizi pamoja na kuonesha dira inayopaswa kufuatwa na Jamii.

Baba Mtakatifu anawahamasisha Maaskofu kushirikiana na Serikali pamoja na vyama vya kiraia, ili kuhakikisha kwamba, utawala wa sheria unazingatiwa kama njia ya ujenzi wa Jamii inayosimikwa katika haki na amani katika kutatua migogoro mbali mbali ya kijamii ili kudumisha amani.

Imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.