Baba Mtakatifu Francisko kwa muda mrefu sasa ameendelea kuwahamasisha waamini kusoma,
kulitafakari na hatimaye kulimwilisha Neno la Mungu kama dira na mwongozo wa maisha
yao ya kila siku. Anawachangamotisha waamini walau kuwa na Biblia ndogo wanayoweza
kuibeba mifukoni mwao, ili kufanya rejea kwa neno la Mungu katika hali mbali mbali
za maisha kwa siku.
Ili kuyaweka mawazo haya katika matendo, Baba Mtakatifu,
Jumapili tarehe 6 Aprili 2014 anatarajiwa kugawa Biblia kwa waamini na mahujaji watakaokuwa
kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, mjini Vatican.
Baba Mtakatifu
Francisko katika ujumbe wake kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii anakiri kwamba,
katika Injili mwamini anaweza kumsikiliza Yesu anayeongea na wafuasi wake. Ni muhimu
ikiwa kama mwamini atajiwekea utamaduni wa kutembea na kujisomea Neno la Mungu kila
wakati anapopata fursa!