2014-04-04 09:22:51

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Tano ya Kipindi cha Kwaresima


Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, tunaendelea na tafakari masomo Dominika ya V ya Kipindi cha Kwaresima. Neno la Mungu latualika kutambua kuwa Kristu ndiye mfalme na chanzo cha maisha yetu. RealAudioMP3

Katika somo la kwanza toka katika kitabu cha Nabii Ezekieli tunakutana na Mungu ambaye anapeleka ujumbe wake kwetu kwa njia ya Ezekieli akisema nitawaondoeni kutoka makaburi yenu na kuwapandisha kwenda nchi ya Israeli. Ezekieli anakuja na habari hii wakati Waisraeli pamoja naye wakiwa utumwani Babeli katika karne ya 6 hivi. Kumbuka Ezekieli alikuwa kasisi aliyepelekwa uhamishoni mnamo mwaka 587KK.

Huko Babeli watu walipata taabu na kukata tamaa na hivi wakawa kama kondoo asiye na mchungaji. Ni kwa sababu hiyo basi Mungu anamtuma Ezekieli kuwatangazia uhuru na kamilisho la ahadi zake, yaani atawarudisha katika maisha mapya, atawatoa katika makaburi yaani toka utumwani na kuwarudisha katika nchi yao.

Ujumbe huu unagusa maisha yetu hivi leo, pale ambapo tunazama katika dhambi na kuacha maisha ya kutimiza mapenzi ya Mungu, tunaingia makaburini. Zaidi ya hilo, vita, madhulumu mbalimbali, uvivu, madawa ya kulevya na magomvi pengine katika familia au katika sehemu zetu za kazi ni alama hakika za utumwa na angamizo la uhuru wetu na hivi kifo. Leo Mungu anatuambia nirudieni mimi nami nitawatoa katika makaburi yenu hayo na kuwarudishia uhai.

Mtakatifu Paulo akiwaandikia Warumi, anawakumbusha wajibu wa kuwa na roho wa Mungu ndani mwao kama kigezo cha kumpendeza Mungu. Ndiyo kusema wale wafuatao matendo ya mwili wako nje ya mstari wa kutimiza mapenzi ya Mungu. Akikazia fundisho hili anasema Kristu aliweza kufufuka kwa sababu alikuwa na roho wa Mungu katika ukamilifu wake.

Ni kwa jinsi hiyo mambo ya kidunia yaani ya kimwili hufa na yatapita lakini yaliyo ya kiroho yaani yaongozwayo na Kristo mwenyewe hayatapita kamwe, bali kuingia katika utukufu wa Mungu kama Kristu mwenyewe alivyoingia. Katika ubatizo tulipokea roho wa Mungu na hivi hata kama maisha yetu yatapita katika ulimwengu huu, lakini haitakuwa mwisho wa kila kitu bali yatageuzwa na kuwa maisha mapya.

Katika somo la Injili mada ni ileile ya yakuwa Bwana ndiye chanzo cha maisha yetu na ndiye atupaye uhai. Bwana atamfufua Lazaro na kumrudishia uhai akithibitisha ukuu wa Mungu na kutaka kujenga imani ya wafuasi wake. Yapo mambo kadhaa ya kuangalia kwa makini katika Injili hii. Jambo la kwanza tunakutana na watu watatu yaani Martha, Mariamu na Lazaro yaani kaka na dada wawili. Hawa ndugu haioneshwi wazazi wao wala ndugu wengine wa karibu, ndiyo kusema tunagundua mwandishi ataka kutuambia juu ya JUMUIYA YA KIKRISTO ambamo hakuna mabwana na watwana, bali wote ni kaka na dada, yaani NDUGU!

Mpendwa msikilizaji, Bwana anapopata taarifa kwamba Lazaro anaumwa haendi huko mpaka atakapofariki na tena baada ya siku nne, Je, alitaka afe? Kwa nini Bwana analia wakati anajua atamwondoa katika mauti Lazaro? Kwa nini Bwana haingia Bethania mara moja? Mpendwa msikilizaji kumwacha Lazaro afe anataka kutufundisha kuwa hakuja kuzuia kifo cha mwili, hakuja kuzuia mtiririko asili wa mambo yamhusuyo mwanadamu, ndiyo kusema hakuja kufanya maisha ya hapa duniani yawe ya milele bali kuyageuza na kuwa maisha mapya yatakayokuwa ya milele.

Kumbe mpendwa msikilizaji, mwili ni lazima utakufa kama njia ya kuingia maisha mapya. Katika hili yafaa kutafakari vema majadiliano kati ya Bwana na Martha ambayo hitimisho lake ni katika maneno ya Bwana akisema “aniaminiye mimi hatakufa kamwe. Bwana anaenda kwa ndugu hawa baada ya siku nne, kwa sababu katika utamaduni wao ilisadikika kwamba katika siku tatu mtu alikuwa hajafa kikamilifu, kumbe ukamilifu wa kifo na ondoko la maisha lilikuwa baada ya siku nne. Lengo la mwinjili ni kutaka kutuambia si jambo jingine bali yakuwa Lazaro alikuwa amepoteza uhai kabisa.

Bwana anapofika katika kaburi la Lazaro analia, na hili linatushangaza kwa sababu alitambua kuwa baada ya muda mfupi atarudisha uhai wake! Katika hali ya kawaida jamaa yetu anapokufa tunalia. Tunalia si kwa sababu ndugu huyu hatafufuka bali kwa sababu kwa kitambo kifupi hatutamwona. Ni alama na ishara ya upendo kwa ndugu zetu. Hata hivyo yafaa kutambua kuwa kuna kilio kilichojaa matumaini kama kilio cha Bwana kwa Lazaro na kilio kisichojaa matumaini, ambacho huona kifo kama mwisho wa kila kitu. Sisi wakristo na watu wenye mapenzi mema yatupasa kulia kama Bwana, tukikazia mapenzi ya Mungu yafanyike na hivi kukazia sala zaidi kwa ajili ya aliyeaga dunia!

Mpendwa msikilizaji, Bwana ataomba liondolewe jiwe juu ya kaburi la Lazaro. Katika utamaduni ule, jiwe lilimaanisha kutenganisha maisha na kifo, dunia ya waliokufa na waliohai, sasa Bwana anataka wakristu waachane na mantiki hii na waishi mantiki ya ufufuko wa Bwana yaani hakuna tena utengano kati yetu na Mungu.

Tukimalizia kujibu swali lisemalo kwa nini Bwana haingia Bethania mara moja, tunaitwa kutambua kuwa Bwana hawezi kuingia katika nyoyo zetu kama zimekata tamaa. Kumbuka, Bethania wanalia kwa sababu ya kifo cha Lazaro na hivi lazima watoke kwanza katika shida hiyo, wajenge tumaini katika Bwana na kisha ataingia katika kijiji chao. Bwana ni maisha, ni tumaini, ni furaha na alipo yeye hakuna kifo, hakuna kilio bali tumaini katika ufufuko.

Mpendwa ninakutakia furaha na matumaini katika maisha yako daima ukimtanguliza Mungu na kwa nguvu zake kukua na kusimamia matumaini na ukuu wa Kristu anayetupatia maisha akituondoa kutoka katika upotofu wa dhambi na kutuingiz katika mwanga wa imani zawadi maisha na uzima wa milele. Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.