2014-04-02 07:28:02

Papa Francisko kukutana na Malkia Elizabeth II mjini Vatican


Malkia Elizabeth wa pili anatarajiwa kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 3 Aprili 2014. Hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa Malkia Elizabeth kukutana na Papa Francisko tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, mwaka mmoja uliopita. Katika Ibada ya Misa Takatifu iliyoadhimishwa na Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 19 Machi 2013, Uingereza ilituma ujumbe kuwakilisha katika tukio hili.

Malikia Elizabeth atakuwa Italia kwa mwaliko kutoka kwa Rais Giorgio Napolitano wa Italia. Ratiba inaonesha kwamba, Malkia pamoja na ujumbe wake, watapata chakula cha mchana kwenye Ikulu ya Italia na baadaye jioni anatarajiwa kukutana na Baba Mtakatifu.

Rais Napolitano alikwishawahi kutoa mwaliko kwa Malkia Elizabeth wa Uingereza kumtembelea, tangu mwaka jana, lakini ilishindikana kutokana na sababu za kiafya. Kumbe, ziara hii inalenga kutekeleza mwaliko kutoka kwa Rais Napolitano pamoja na kukutana na Baba Mtakatifu Francisko.

Kumbu kumbu zinaonesha kwamba, Malkia Elizabeth wa Uingereza alibahatika kukutana na kuzungumza na Mwenyeheri Yohane Paulo II mjini Vatican kunako tarehe 17 Oktoba 2000 wakati wa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka Elfu mbili ya Ukristo.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI alikutana na kuzungumza na Malkia Elizabeth wa Uingereza mjini London, wakati wa hija yake ya kitume iliyofanyika mwezi Septemba 2010. Kumbu kumbu zinaonesha pia kwamba, Malkia Elizabeth aliwahi kukutana na Papa Yohane wa XXIII kunako Mwaka 1961.








All the contents on this site are copyrighted ©.