2014-04-02 10:26:04

Mataifa makubwa yanavyomezea utajiri wa Bara la Afrika!


China na Japan ni kati ya mataifa makubwa yanayoendelea kunyemelea utajiri wa rasilimali kutoka Barani Afrika, China ikiongoza kwa kuwekeza kwa wingi zaidi na sasa Japan imeanza pia kuamka. Safari ya kikazi barani Afrika iliyofanywa mwezi Januari na Waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe, ulikuwa ni mwanzo wa Japan kutaka kuwekeza katika nishati Barani Afrika. Hii ni vita ya kidiplomasia na safari ya utafutaji wa nishati ya mafuta Barani Afrika kama vyombo vya habari vinavyofafanua hali hii nchini Japan.

Waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe, katika safari yake ya kikazi, alitembelea Pwani ya Pembe. Ethiopia na Msumbiji ambako hivi karibuni kumegunduliwa madini yanayoweza kutumika katika nishati kwa kipindi cha miaka ishirini. Japan inataka kuwekeza katika nishati nchini Msumbiji kwa kushirikiana na Brazil. Mradi wa "Pro Savana umepewa ekari millioni kumi na moja za ardhi kwa ajili ya kilimo cha nafaka. Japan pamoja na mambo mengine inataka pia kuwekeza katika nishati na miundo mbinu kama sehemu ya mchakato wa maboresho ya maisha ya wananchi wa Msumbiji.

Wachunguzi wa mambo wanasema, kuna raia millioni moja kutoka China wanaoishi na kufanya kazi Barani Afrika na kwamba, wamewekeza kiasi kikubwa cha fedha katika shughuli za uzalishaji, ikilinganishwa na Japan. Lakini, Japan inataka kuongeza kasi katika uwekezaji Barani Afrika na tayari katika kipindi cha miaka mitano itatoa kiasi cha dolla za Kimarekani billioni mbili zitakazolipwa kwa riba kidogo, ili sekta ya binafsi iweze kupata uwezo mkubwa zaidi wa kiuchumi.

Mambo si haba kutokana na kugunduliwa kwa nishati Barani Afrika kwani hata nchi za Ulaya zinamezea mate nishati na madini kutoka Barani Afrika, kama ambavyo hivi karibuni Kampuni ya mafuta ya Total kutoka Ufaransa imetiliana sahihi mkataba na Serikali ya Uganda tayari kuanza biashara ya mafuta kutoka Uganda. Ni matumaini ya wananchi wa Bara la Afrika kwamba, wataweza kufaidika na rasilimali hii inayogambaniwa na Mataifa makubwa duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.