2014-04-02 09:44:15

Jrs, Syria mshindi wa tuzo ya amani kwa Mwaka 2014


Shirika la Kitume Kimataifa la "Pax Christi" limelitunukia Shirika la Wayesuit la kuhudumia Wakimbizi, Syria, Jrs, tuzo la amani kwa Mwaka 2014 kutokana na mchango wake mkubwa katika kuwahudumia wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum nchini Syria tangu mwaka 2011, vita ilipofumuka nchini Syria.

Tuzo hili lilianzishwa kunako Mwaka 1988 kutokana na Mfuko wa Amani wa Kardinali Bernardus Alfrink na unatoa tuzo kwa kuthamini mchango unaotolewa na watu binafsi, vikundi na mashirika mbali mbali katika mchakato wa kulinda na kudumisha: haki na amani sehemu mbali mbali za dunia.

Shirika la Wayesuit la kuhudumia Wakimbizi tangu mwaka 2008 limekuwa mstari wa mbele katika kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji kutoka Kaskazini mwa Afrika na huko Mashariki ya Kati. Kwa namna ya pekee, kunako Mwaka 2001, Jrs ilijielekeza zaidi kwa ajili ya kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji kutoka Syria, kwa kutoa huduma ya tiba, elimu na maendeleo. Jrs linaendesha pia kampeni ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa.

Jrs kwa sasa linaendelea kutoa msaada wa chakula kwa maelfu ya wahamiaji na wakimbizi kutoka Syria pamoja na kuwapatia msaada wa tiba na elimu kwa watu zaidi ya 9, 800. Kuna jumla ya watu laki tatu wanaohudumiwa na Jrs kutoka Syria. Tuzo hii itatolewa hapo tarehe 8 Juni 2014 huko Sarayevo.







All the contents on this site are copyrighted ©.