Ukweli utawaweka huru ndiyo kauli mbiu inayoongoza ujumbe wa Kwaresima kwa Mwaka 2014
kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania. Katika ujumbe huu, Maaskofu wanapembua
maana ya wongofu wa kweli unaowaweka huru; wajibu wa kuuishi, kuulinda na kuusimamia
ukweli kishuhuda.
Baraza la
Maaskofu Katoliki limeangalia hali halisi ilivyo nchini Tanzania. Sehemu hii ya mwisho,
tunapenda kukushirikisha mambo yanayovuruga amani na utulivu nchini Tanzania, kama
yalivyobainishwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika ujumbe wao wa Kwaresima.
Uvunjifu wa amani
Taifa letu linazidi kupoteza tunu bora ya amani ambayo
waasisi wa taifa letu wametuachia. Katika siku za karibuni yamekuwepo matukio ya mauaji,
watu kumwagiwa tindikali kwa sababu ya imani yao au visasi na hata mauaji kwa kutumia
mabomu. Uhasama wa kidini na matukio ya kijasusi na ugaidi dhidi ya raia yanaonekana
kushamiri. Kumekuwapo na matumizi makubwa ya nguvu upande wa vyombo vya dola vikitumia
silaha za moto na za kivita. Wimbi la wananchi kutotii sheria na taratibu za nchi
linakua. Tunakwenda wapi?
Amani lazima ilindwe ndani na nje ya mipaka ya nchi
yetu. Hata hivyo, amani sio tunu inayojitegemea peke yake kwa kuwa amani ya kweli
inazaliwa ndani ya mioyo yenye kujali misingi ya utu, haki, heshima, ukweli na umoja.
Fikra tofauti na hizo, huzaa mioyo potofu, na mioyo potofu haiwezi kutoa amani. Rushwa
na madawa ya kulevya
Mapambano dhidi ya rushwa na madawa ya kulevya yamegeuka
kuwa wimbo unaochosha kwa sababu hakuna dhamira ya dhati ya kuitokomeza. Uongozi wa
juu unapotamka hadharani kuwafahamu watoa rushwa, wapokea rushwa na wafanyabiashara
wa madawa ya kulevya lakini hakuna hatua zozote zinazochukuliwa ni hali inayotisha
sana. Wakati umefika ambapo lazima tuwe wakweli kuhusu mapambano dhidi ya rushwa na
madawa ya kulevya. Hatuwezi kuwa huru kuhusu rushwa na madawa ya kulevya kama hatujawa
wakweli kuhusu mapambano dhidi ya rushwa na madawa ya kulevya. Wanaopiga vita rushwa
majukwaani, ndio wanaoomba na kupokea nje ya jukwaa. Isitoshe rushwa ndiyo ngazi waliyoitumia
na wanayoitumia kufika jukwaani. Katika mazingira kama haya hatujengi Taifa bali tunalibomoa
na historia itatuhukumu. Hatuna budi kuunda misingi imara ya utawala bora. Tukumbuke
daima kuwa utawala bora bila uwajibikaji na kuwajibishana ni kiini macho. Kukua
kwa matabaka katika jamii
Tofauti kubwa sana za kiuchumi zinazidi kupanua utengano
wa kimatabaka kati ya wenye nguvu za kiuchumi na wasio na kitu. Wenye nguvu kiuchumi
sasa wanamiliki uchumi, wanamiliki siasa na hatima ya fukara, na kwa fedha wananunua
haki ya wanyonge.
Mgawanyo mbovu wa rasilimali za nchi unatisha. Ardhi
inamilikiwa na wachache kwa kivuli cha uwekezaji mkubwa huku wananchi wakiahidiwa
ajira kwa kuwa vibarua kwenye mashamba hayo badala ya kuwezeshwa kumiliki ardhi na
kuitumia kwa faida. Haya ni masuala yanayomtia hofu mtu yeyote anayejali na kuthamini
mustakabali wa taifa letu. Siasa kuingilia weledi
Tatizo la siasa kutawala
mifumo ya ujenzi wa misingi ya maendeleo linakua kwa kiwango cha kutia hofu. Kwa mfano,
siasa na wanasiasa wanaathiri mfumo wa utoaji wa elimu nchini kiasi cha kulifanya
taifa hili kuwa kama taifa lisilojali mustakabali wake. Yamekuwepo maneno mengi na
mipango ya zimamoto isiyofanyiwa utafiti wa kina na utendaji umekuwa hafifu sana.
Uthabiti katika kusimamia utekelezaji wa mipango ya maendeleo hauonekani na badala
yake porojo zimetawala. Imejitokeza hali ya wale waliopewa dhamana ya kusimamia masuala
ya elimu kwa mfano kukosa unyenyekevu wa kuwasikiliza na kushauriana na wataalamu
katika nyanja hizi. Kila mara zinaibuka sera ambazo msingi wake ni ubunifu usiozingatia
weledi na hivi kuifanya elimu kudidimia. Mchakato wa Katiba mpya
Katiba
kama moyo wa taifa ni chombo kinachopaswa kutengeneza misingi ya mfumo wa maisha mazima
na uhai wa Taifa letu. Ukweli wote na uhuru wote wa Taifa unabebwa na Katiba. Iwapo
mchakato wa katiba mpya hautaendeshwa kwa ukweli na uhuru, hatutaweza kupata katiba
yenye kubeba ukweli na uhuru wote kuhusu taifa letu. Tunarudia tena kutamka kuwa zoezi
hili adhimu na la muhimu kwa mustakabali wa Taifa limeharakishwa mno. Sasa tunaona
zoezi zima limehodhiwa na wanasiasa. Mchakato wa katiba mpya unadai kuwepo kwa fadhila
ya kijamii ya kutafuta manufaa ya wote (common good). Katiba si mali ya wanasiasa
bali ni mali ya wananchi. Tunapenda kuialika jamii yote kuitendea haki nchi yetu.
Tukae chini na tuzipime kila hatua zetu katika zoezi hili na tuone kama zinakidhi
kipimo cha «Hekima, Umoja na Amani». Hekima ituongoze kulinda umoja wa Taifa letu
na utuepushe na kishawishi cha kubaguana na kutengana. Kwa kuzingatia hilo umoja huo
utatuongoza katika njia ya amani.
Uharibifu wa mazingira
Tishio kubwa
la kimaangamizi kwa vizazi vijavyo linatokana na ukweli kuwa kumekuwepo na uharibifu
mkubwa wa mazingira. Maendeleo yanagharama yake. Kiu ya kweli ya maendeleo ni lazima
iambatane na ulazima wa kuwa makini katika kutunza mazingira na uthabiti wa uumbaji.
Vyanzo vya maji na kingo za mito zimeharibiwa kwa kuruhusu shughuli za kilimo kufanyikia
maeneo hayo, kwa kuruhusu makazi ya watu, viwanda kujengwa na kuruhusu takataka ya
sumu kutoka viwandani na migodini kutiririkia kwenye vyanzo vya maji, nk. Ukataji
wa miti umeshamiri na baadhi ya misitu ya asili imepotea. Kwa sababu hiyo tumechangia
sana katika kusababisha mabadiliko ya tabia nchi ambayo athari zake sasa zinajionesha
waziwazi. Ukame, njaa, mafarakano kati ya wakulima na wafugaji na kuenea kwa jangwa
ni vitisho vilivyo dhahiri mbele yetu. Huu ni ukweli kuwa tumeshindwa kuzingatia agizo
la Mungu la kuitawala na dunia kuutiisha ulimwengu. Tunahitaji sasa kubadilika ili
ukweli utawale, tupate uhuru kamili kwa kuwajibika kuyalinda na kuyatunza mazingira
kwa faida ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo. Ni wajibu wetu Waamini Wakatoliki
kuulinda ukweli na kuusimamia kiushuhuda. Jitahada za namna hii zina gharama yake
kwa kuwa zinahitaji ujasiri wa kinabii na utayari wa kuteseka na hata ikibidi kutoa
sadaka kubwa ya uhai. HITIMISHO
Wapendwa Taifa la Mungu, tunapenda kuwahimiza
kwa maneno haya tukisema: “Inunue kweli, wala usiiuze. Naam, hekima na mafundisho
na ufahamu” (Mith 23:23). Ukweli ni msingi wa lazima na unapaswa kuwa wa kudumu kwa
tendo lolote ili liweze kuitwa kuwa ni adilifu. Ukweli unapaswa kuzijenga dhamiri
zetu ili kumsaidia mwanadamu kupata mwanga unaofukuza mikanganyiko.
Katika
ulimwengu usiojali ukweli, uhuru unapoteza msingi wake na mwanadamu anakuwa mhanga
wa vurugu ya vionjo na kutawaliwa kwa hila, iliyojidhihirisha waziwazi au iliyojificha.
Hivi ni mwaliko kwetu sote “tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye
katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo” (Efe 4:15). Kwa sababu upendo “haufurahii
udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli” (1Kor 13:6).