Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amewataka wanawake walioteuliwa kwenye Tuzo
ya Mwanamke Bora wa mwaka 2013/2014 wasibweteke bali waendeleze juhudi zao na wazidi
kung’ara zaidi. Ametoa wito huo Jumamosi usiku, Machi 29, 2014 kwenye hafla ya kumtuza
mwanamke bora wa mwaka 2013/2014 iliyofanyika kwenye ukumbi wa African Dream nje kidogo
ya mji wa Dodoma.
“Lazima muendelee kuonekana mnazidi kung’ara. Tuzo ni njema
kwa upande mmoja lakini pia ina changamoto zake kubwa ikiwa ni ya kuendelea kubaki
mnang’ara hadi waliowapigia kura wakawaona mnafaa,” alisema Waziri Mkuu. Utoaji wa
tuzo hiyo uliwapambanisha Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna
Tibaijuka; Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro; Mwalimu Mkuu Mstaafu
na Mbunge Mstaafu, Dk. Maria Kamm pamoja na Mbunge wa Same Mashariki, Bi. Anne Kilango
Malecela.
Kila mmoja alikabidihiwa Tuzo ya Mwanamke Bora na Waziri Mkuu Pinda
lakini Dk. Maria Kamm ndiye aliyeibuka mshindi wa jumla kwa kukabidhiwa medali maalum
pamoja na hundi ya sh. milioni tano. Waziri Mkuu alipongeza Mkurugenzi Mtendaji wa
kampuni ya Global Publishers, Bw. Eric Shigongo kwa kuthamini mchango wa wanawake
katika jamii na kuanzisha wazo la kutoa tuzo hiyo.
Alimtaka Bw. Shigongo aangalie
uwezekano wa kuiendesha tuzo hiyo iendane na maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani
ambayo huadhimishwa Machi 8, kila mwaka. “Kabla ya siku hiyo, kuwe na wiki nzima ya
maadhimisho, iendeshwe mijadala kuhusu shughuli za wanawake, mada zinazohusu masuala
hasi na chanya ya wanawake zitolewe,” alisema.
“Ningependa kuona viongozi
wa Kitaifa wakiibeba Wiki ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake kama njia ya kutambua
mchango wa wanawake kwenye Taifa hili. Tunao mwaka mzima wa kujiandaa kwa ajili ya
jambo hili, tutashirikiana kadri inavyowezekana,” alisisitiza. Wanawake waliopewa
tuzo walimshukuru Bw. Shigongo kwa kutambua jitihada za wanawake mbalimbali hapa nchini
na kuamua kuazisha tuzo hiyo.