2014-03-31 08:54:38

Maaskofu Katoliki Tanzania kuanza hija ya kitume mjini Vatican:Tarehe 4-7 Aprili 2014


Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 7 Aprili 2014 watakuwa na hija ya kitume na kikanuni mjini Vatican, hija ambayo kimsingi inapaswa kufanyika walau kila baada ya miaka mitano. RealAudioMP3

Katika mahojiano maalum na Radio Vatican, Padre Raymond Saba, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anasema kwamba, hija ya Maaskofu ni kielelezo cha mshikamano wa umoja wa Kanisa la Kiulimwengu na Makanisa mahalia. Hii ni fursa kwa Maaskofu kutembelea na kuhiji kwenye makaburi ya miamba wa imani; yaani Mtakatifu Petro na Paulo yaliyoko mjini Vatican pamoja na kukutana na viongozi wa Mabaraza ya Kipapa.

Kilele cha hija ya Maaskofu ni kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko, ili kwa pamoja kuweza kujadili: maisha, utume, changamoto na matarajio ya Kanisa la Tanzania kwa siku za usoni. Itakumbukwa kwamba, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania lilifanya hija ya kitume na kikanuni kwa mara ya mwisho kunako mwaka 2005, wakati Mwenyeheri Yohane Paulo II alipokuwa amelazwa kwenye Hospitali ya Gemelli. Wao wakawa ni Maaskofu wa mwisho kama Baraza kuweza kukutana na Papa Yohane Paulo II.

Padre Raymond Saba anasema, kimsingi hija ya kitume inapania pamoja na mambo mengine kudhihirisha imani kama Baraza la Maaskofu wa Tanzania wakiwa wameungana na Baba Mtakatifu Francisko.







All the contents on this site are copyrighted ©.