Kifo hakizoeleki, tubuni na kuongoka msijidanganye kwamba muda bado!
Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro, mwishoni mwa juma ameongoza Ibada
ya Misa takatifu kwa ajili ya mazishi ya aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mara John Tuppa
aliyefariki dunia hivi karibuni akiwa kazini. Askofu Mkude amewataka watu waliohudhuria
mazishi hayo kufanya toba na wongofu wa ndani kama njia ya kuleta mabadiliko kwenye
maisha yao.
“Ninawaomba kila mmoja mahali hapa afanye toba, awe mkweli, asifanye
uchakachuaji... kila mtu kwa imani yake aache mabaya na atende mema kama ndugu yetu
John Tuppa ambaye alijitoa na kufanya zaidi kwa ajili ya wengine,” alisema. Aliwataka
watu wote wajihoji njia zao kama ni kamilifu, na kwamba ni kwa vipi wanawatendea watu
wengine wanaohusiana nao iwe ni baba, mama, watoto au hata maofisini na kwenye biashara.
“Je
mnawaongozaje watu katika ofisi zenu katika ngazi mbalimbali, iwe ni wizarani, mkoani,
wilayani hadi kwa mtendaji wa kijiji? Je, unawafanyaje watu katika biashara unayofanya?
Je unawadhalilisha kwa kuwauzia vitu vibovu? Je, unawauzia madawa ya kulevya?” alihoji
Askofu Mkude. Aliwataka watu wote kila mmoja kwa imani yake waendelee kuuombea mchakato
wa Katiba ili iweze kupatikana Katiba bora zaidi. “Tuna wajibu kama wacha Mungu tuwaombee
wajumbe wa Bunge maalum ili kazi ile ifanyike sawa na mapenzi ya Mungu. Tusipowaombea
watafanya vitu vya ajabu,” alisisitiza.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mahusiano),
Bw. Stephen Wassira aliwavunja mbavu waombolezaji waliofika kwenye mazishi ya aliyekuwa
Mkuu wa Mkoa wa Mara marehemu John Gabriel Tuppa yaliyofanyika nyumbani kwake Kilosa
mjini, mkoani Morogoro.
Akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya wabunge wa
mkoa wa Mara, Bw. Wassira alisema watu wote waliohudhuria mazishi hayo wanataka kwenda
peponi lakini tatizo ni masharti yanayoambatana na hiyo safari. “Baba Askofu Mkude
(Telesphor), ukiuliza nani anataka kwenda peponi, wote hapa watanyoosha mikono, lakini
tatizo ni masharti yanayoambatana na safari ya kwenda huko peponi. Kila mtu anaona
ugumu wa hayo masharti ukiwemo wewe Baba Askofu,” alisema huku umati uliokuwepo ukiangua
vicheko.
Alisema kifo hakizoeleki wala hakizuiliki na kwamba hakuna anayeweza
kuchakachua siri ya Mwenyezi Mungu kuhusu uhai wa maisha ya wanadamu. Aliwaombea wafiwa
wapate faraja katika kipindi hiki kigumu.
Akizungumza na waombolezaji wakati
wa ibada ya mazishi nyumbani kwa marehemu, Jumamosi, jioni Machi 30, 2014, Waziri
Mkuu Mizengo Pinda alisema amemfahamu marehamu Tuppa tangu mwaka 1993 alipoteuliwa
kuwa Mkuu wa Wilaya kwa mara ya kwanza.
“Marehemu Tuppa amekuwa mtumishi Serikalini
kwa muda wa miaka 42 na katika muda wote huo, miaka 21 ya utumishi wake ameitumia
akihudumia wananchi kama Mkuu wa Wilaya na Mkuu wa Mkoa. Alikuwa ni mtu mwema, aliyejali
watu na wala hakuwa na tamaa za hovyo hovyo,” alisema Waziri Mkuu.
“Kumpoteza
mume na baba ni mtihani mkubwa lakini mkimtumaini Mwenyezi Mungu mtafaulu,” alisema
Waziri Mkuu na kuwasihi mjane wa marehemu Tuppa pamoja na watoto wasisononeke wanapopatwa
na jambo na wala wasisite kumuona Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, yeye binafsi ama Rais
Jakaya Kikwete kwa msaada zaidi.
Mazishi hayo yalihudhuriwa pia na Makamu wa
Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal, baadhi ya mawaziri, wabunge wa mikoa ya Mara na Morogoro,
wakuu wa mikoa mbalimbali, viongozi wa dini na viongozi wa vyama vya siasa.
Bw.
Tuppa alizaliwa Januari mosi, 1950. Amewahi kuwa Mkuu wa Wilaya za Chunya, Mwanga,
Bukoba, Muleba na Dodoma kabla ya kuteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Mara mwaka 2011.
Ameacha mjane, watoto watano na wajukuu watano.