2014-03-29 08:40:16

Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa si tiketi ya kuelekea kaburini!


Kwa njia ya Sakramenti za kuingizwa katika Ukristo, mtu hupokea uzima mpya wa Kristo unaochukuliwa katika vyombo vya udongo nao hubaki umefichika pamoja na Kristo. Mwanadamu yumo duniani akielemewa na hali ya mateso, magonjwa na kifo. Uzima mpya wa watoto wa Mungu unaweza kudhohofika na hata kupotezwa kwa dhambi.

Mama Kanisa anafundisha kwamba, Yesu Kristo ni mganga wa roho na miili; alisamehe dhambi na kuwarudishia watu afya ya miili. Ni kwa njia ya utashi wa Yesu mwenyewe kwamba, Kanisa kwa nguvu ya Roho Mtakatifu liendeleze kazi ya uponyaji na wokovu hata miongoni mwa viungo vyake. Hili ndilo lengo kuu la Sakramenti za Uponyaji, yaani Sakramenti ya Kitubio na Mpako wa Wagonjwa.

Kwa mpako mtakatifu wa wagonjwa na sala za makuhani, Kanisa lote huwakabidhi wagonjwa kwa Bwana aliyeteswa na kutukuzwa ili awainue na kuwaokoa. Kanisa linawahimiza wagonjwa kujiunga kwa hiari na mateso na kifo cha Kristo ili kuchangia mafao ya Taifa la Mungu. Pamoja na Katekesi ya kina, waamini wengi wamekuwa na woga wa kupokea Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa, wakidhani kwamba, hiyo ni tikeketi ya kuwapeleka kaburini.

Baraza la Maaskofu katoliki Senegal kwa kutambua umuhimu wa Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa, Jumapili tarehe 30, 2014 linafanya semina maalum ili kutambua kwa mara nyingine tena umuhimu wa Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa, ili waamini wengi waweze kukimbilia huruma na upendo wa Mungu katika mahangaiko yao wakati wanapokuwa katika Altare ya mahangaiko ya binadamu. Sakramenti ya Mpako wa Wagonjwa, ipewe hadhi yake hasa na wafanyakazi katika Sekta ya Afya na waamini katika ujumla wao.

Siku hii inapambambwa kwa tafakari za kina kutoka kwa wadau mbali mbali katika shughuli za kichungaji kwa wagonjwa, Ibada ya Misa Takatifu pamoja na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.